Ruge Mutahaba afariki dunia, Rais Magufuli amlilia

Muktasari:

  • Rais wa Tanzania, John Magufuli amesema amesikitishwa na kifo cha Mkurugenzi wa Vipindi wa Clouds Televisheni na Radio, Ruge Mutahaba aliyefariki leo Jumanne.

Dar es Salaam. Mkurugenzi wa vipindi kutoka Clouds Media Group, Ruge Mutahaba amefariki dunia leo Februari 26, 2019 hospitali alikokuwa akipatiwa matibabu.

Taarifa za kupoteza maisha kwa Ruge zimetangazwa katika taarifa ya habari ya ITV huku Rais John Magufuli akituma salamu za pole kwa wafiwa kupitia akaunti yake ya Twitter.

Ruge alikuwa akisumbuliwa na maradhi ya figo na kulazwa hospitali nchini Afrika kusini kwa miezi kadhaa.

Kupitia akaunti yake ya Twitter, Rais Magufuli ameandika, “Nimepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha kijana wangu, Ruge Mutahaba.”

“Daima nitamkumbuka kwa mchango wake mkubwa katika tasnia ya habari, burudani, na juhudi za kujenga fikra za maendeleo kwa vijana. Poleni wanafamilia, ndugu, jamaa na marafiki. Mungu amweke mahali pema, Amina.”