Fanyeni haya mtapata raha mkiwa faragha

Mwanakwetu ni jambo rahisi sana kukutana kimwili na mwenza wako, jambo gumu na linalowashinda wengi ni kujipa raha wewe mwenyewe na mwenza wako kwa wakati mmoja.

Hii husababisha wenza wengi kupoteza hamu ya kukutana na wenza wao faragha kutokana na kuchoka kufanya kazi ya bure ambayo haiwaburudishi. Kwa wasiokuwa na staha hutafuta wenza nje ya uhusiano wao.

Pamoja na kuwa na gari, nyumba nzuri na kazi inayokulipa vizuri, kama hupati au humpi mwenzako raha ya tendo la ndoa, hivyo vyote ni kazi bure.

Kuna vitu vingi vitakavyosaidia kupata raha mnayoikusudia wote ila jitahidi haya manne yasikose.

Maandalizi

Tendo la ndoa siyo jambo la kukurupuka kama unataka kulifurahia kwa muda mrefu.

Hivyo kabla ya kuingia mchezoni hakikisheni mmefanya maandalizi ya kimwili na kiakili.

Pia eneo mtakalobanjuliana liwe safi na lenye stara, litakalowapa uhuru wa kujiachia mtakavyo ikiwamo miguno, kelele kutosikika.

Usifanye peke yako

Raha ya tendo hili ni kujumuika wawili tena kwa ushirikiano wa hali ya juu, hivyo kabla ya kuanza ujue unapaswa kushirikiana na mwenzako bega kwa bega.

Ukitosheka hakikisha na mwenzako ametosheka hata kama umechoka...hili linawashinda wengi hivyo unapojipanga kwa ajili ya kula tunda hakikisha hili lipo akilini.

Mwanaume siyo kazi yake kukufurahisha wewe peke yako na wala mwanamke siyo jukumu lake kukuburudisha wewe peke yako, hivyo burudishaneni. Hakika kuburudishana ndiyo jambo pekee lililowaweka pamoja na si kupika, kufua wala uzuri.

Jifunze mipigo mipya

Usijifunze kila kukicha, lakini hakikisha unajua mipigo mipya ya kujamiiana na mwenza wako, badala ya kusubiri yeye aje na mpya na kujikuta unakuwa mgeni.

Kuwa na mitindo mipya kutakusaidia siyo tu kumfanya mwenza wako awe na hamu ya kukutana na wewe kimwili mara nyingi, bali utakuwa na fursa ya kuutawala mchezo.

Faida nyingine ya kuwa na mipigo mipya itakuongezea kujiamini na ukijiamini bila shaka hutafanya makosa.

Usijibane jieleze

Mwisho na muhimu usijibane mweleze mwenza wako anakokufikisha, lalamika kimahaba ili umuongezee hamu na gamu ya kuendelea kuburudishana.

Kukaa kimya kwenye tukio hilo ni kulipunguzia ladha, kama wewe hupendi inawezekana mwenza wako anapenda, hivyo jitahidi kulipa uhai tukio hilo badala ya kukaa kimya kama unafanyiwa upasuaji.

Ukiguswa sehemu unayofurahia hakikisha anajua ama kwa kutoa sauti ya juu kidogo (siyo yowe yaani itofautiane na ile uliyokuwa ukiitoa mwanzo) au kumshika kwa nguvu.

Hii siwaambii wanawake hata nyinyi wanaume wenza wenu wanataka kujua kama mmekolea au laa.

Jitahidi kuugulia jamani kwa sababu siyo dhambi, kama unashindwa basi gugumia hata kidogo.

Tunajuzana jamani siyo kwa ubaya, faragha ni jambo la maana kuliko mengine mengi myafanyayo lipeni umuhimu wa kipekee kwa kulifanya liwe live.