Meneja azungumzia Ommy Dimpoz kuwa ICU

Ommy Dimpoz

Muktasari:

Ommy Dimpoz alifanyiwa upasuaji wa koo miezi minne iliyopita.

Dar es Salaam. Uongozi wa Rockstar 4000 umesema taarifa zilizosambaa katika mitandao ya kijamii kuwa msanii,  Omary Nyembo maarufu Ommy Dimpoz kuwa amelazwa hospitali katika chumba cha uangalizi maalum (ICU) hazina ukweli wowote.

Kauli hiyo imetolewa baada ya taarifa za kulazwa kwa msanii huyo kusambaa  huku baadhi ya wasanii wakiweka picha yake na kusema hali yake kwa sasa ni mbaya.

Akizungumza na MCL Digital leo Jumamosi Agosti 25, 2018, meneja wa msanii huyo Seven Mosha amesema hali ya msanii huyo kwa sasa inaendelea vizuri.

Amesema Ommy Dimpoz alifanyiwa upasuaji wa koo miezi minne iliyopita na tangu hapo hali yake imekuwa ikiendelea vizuri hadi sasa.

“Juzi alikwenda hospitali kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi kwa kuwa kila baada ya miezi mitatu anatakiwa kurudi hospitali ili kuangalia maendeleo yake kama tulivyoelekezwa na madaktari,” amesema Mosha.

Alipoulizwa kuhusu taarifa zinazosambaa kuwa amelazwa ICU, Seven amesema hazina ukweli.

“Dimpoz ni mzima wa afya na hajalazwa, yupo nyumbani baada ya uchunguzi,” amesema na kusisitiza kuwa madaktari kutoka Hospitali ya Milpark iliyopo nchini Afrika Kusini wanamhudumia vyema.

Mwanamuziki Madee leo katika ukurasa wake wa Instagram aliweka picha ya Ommy Dimpoz na kuandika, “Kwenye maombi yetu ya kila siku tusimsahau Omary .. tumuombee apone haraka aendelee na majukumu yake ,Omary anaumwa. Tuseme Amen.”

Mtangazaji wa kipindi cha Shilawadu, Soudy Brown naye ameandika, “Omary upo ICU? Haiwezekani huko sio kwako fight, pona mzee baba, pona uje shilawadu tukutoe povu kama zamani, pona urudi gym kama zamani, pona urudi jukwaani kama zamani, pona uje u record mangoma kama zamani.”