Shahidi : Nilimpigia kura Lema ingawa mimi ni mwanaCCM

Muktasari:

Rajab aliieleza Mahakama hiyo kuwa alipofika katika mkutano huo alishtuka kusikia maneno yakitamkwa na mbunge wake yanayosema Rais Magufuli anabana demokrasia na kwa kubana demokrasia atasababisha umwagaji wa damu.

Moses Mashalla, Mwananchi [email protected]

Arusha. Shahidi wa pili katika kesi ya kudaiwa kumdhalilisha Rais John Magufuli inayomkabili mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema ameieleza Mahakama ya Wilaya ya Arumeru kuwa ingawa yeye ni mwanachama wa CCM, mwaka 2015 kwenye Uchaguzi Mkuu alimpigia kura mshtakiwa huyo.

Shahidi huyo Masoud Rajab (41) mkazi wa Kata ya Muriet aliieleza Mahakama kuwa Juni 22 2016 akiwa mwanachama wa CCM alihudhuria mkutano uliotishwa na mbunge huyo kama mwananchi wa kawaida.

“Sina kumbukumbu na nambari ya kadi yangu ya CCM na sikumbuki niliichukulia wapi, lakini mwaka 2015 nilimpigia kura Lema,” alisema shahidi huyo.

Akijibu swali aliloulizwa na wakili wa upande wa utetezi, John Mallya kwamba alikwenda kutafuta nini katika mkutano huo uliofanyika Kata ya Ngarenaro ihali yeye ni mkazi wa Muriet, alisema alipata taarifa kuwa kuna mkutano.

Rajab aliieleza Mahakama hiyo kuwa alipofika katika mkutano huo alishtuka kusikia maneno yakitamkwa na mbunge wake yanayosema Rais Magufuli anabana demokrasia na kwa kubana demokrasia atasababisha umwagaji wa damu.

Alidai maneno mengine aliyosikia ni kwamba endapo ataendelea watu vifua vitawajaa na ipo siku vitalipuka na siyo jeshi au polisi wataweza kuzuia.

Akijibu swali kutoka kwa wakili Mallya kwamba anaelewa nini kuhusu maneno vifua vitawajaa na umwagaji wa damu, shahidi huyo alisema anaelewa ni hasira na kuchuruzika kwa damu.

Rajab alidai kuwa baada ya kusikia kauli ya umwagaji wa damu, alikosa amani na kuamua kwenda kituo kikuu cha polisi saa mbili usiku kufungua jalada la mashtaka.