Sumaye apewa notisi ya siku 90 kuendeleza mashamba

Waziri mkuu mstaafu, Frederick Sumaye

Muktasari:

Sumaye, ambaye alikuwa mmoja wa wasemaji tegemeo kwenye mikutano ya kampeni za Uchaguzi Mkuu uliopita ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), anamiliki shamba lililoko mkoani Morogoro na jingine lililoko Mabwepande jijini Dar es Salaam, ambalo limevamiwa na wananchi.

Dar es Salaam. Serikali imemtaka Frederick Sumaye kuendeleza mashamba yake mawili ndani ya siku 90, la sivyo itafuta hati ya umiliki wake, lakini waziri mkuu huyo mstaafu amesema notisi hiyo ni matokeo ya chuki ya Serikali dhidi yake baada ya kuhama CCM na kujiunga Chadema.

Sumaye, ambaye alikuwa mmoja wa wasemaji tegemeo kwenye mikutano ya kampeni za Uchaguzi Mkuu uliopita ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), anamiliki shamba lililoko mkoani Morogoro na jingine lililoko Mabwepande jijini Dar es Salaam, ambalo limevamiwa na wananchi.

Waziri wa Ardhi, William Lukuvi alisema hati ya shamba la Sumaye iko katika hatua ya kufutwa na kwamba Ofisa Ardhi Mteule wa Wilaya ya Kinondoni, Rehema Mwinuka ameshatoa barua ya notisi.