Mkazi wa Manzese ashinda Sh20 milioni za Tigo

Dar es Salaam. Salum Biwi (32) mkazi wa Manzese jijini Dar es Salaam ameibuka mshindi wa kwanza wa kampeni ya ‘Kishindo cha Funga Mwaka’ inayoendeshwa na Kampuni ya Tigo na kujinyakulia kiasi cha Sh20 Milioni.

 

Promosheni hiyo pia imeshuhudia washindi wengine wawili akiwamo Hamidu Mtabiage (32) mkazi wa Lindi alieshinda Sh15 milioni na Anna Mkongwa (32) kutoka Dodoma ambaye ameshinda Sh10 milioni kama sehemu ya washindi watatu wa jumla.

 

Akizungumza mara baada ya kupigiwa simu ili kumfahamisha kuhusu ushindi huo, Biwi alisema amepokea kwa furaha ushindi huo huku akiishukuru Tigo kwa kuja na promosheni hiyo ambayo imemfanya kufunga mwaka kwa kishindo.

 

“Nimekuwa nikiweka pesa na kupokea pesa kwenye namba yangu ya Tigo Pesa na sikutegemea kama ningeshinda kiasi hiki cha fedha, nawashukuru sana Tigo kwa kampeni yao hii ambayo imenifanya nimalize mwaka vizuri zaidi,” alisema Biwi ambaye ni mtaalamu wa masoko.

 

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Tigo Pesa, Angelica Pesha alisema Kampeni hiyo iliyodumu kwa mwezi mmoja ilikuwa na lengo la kuwawezesha wateja wanaoweka au kupokea pesa kwa njia ya Tigo Pesa kufunga mwaka kwa kishindo.

 

“Kampeni hii ilitenga jumla ya Sh500 milioni kwaajili ya wateja zaidi ya 331 wanaoweka na kupokea pesa kwa njia ya Tigo Pesa na hatimaye leo imeweza kufikia kikomo kwa kuwapata washindi watatu wa jumla,” alisema.

 

Mbali na washindi hao, Kampeni hiyo ilikuwa ikitoa zawadi kwa washindi 8 wa Sh1 milioni kila siku na washindi 8 wa Sh5 Milioni kila wiki na tayari wamekwisha pokea zawadi zao.

 

“Wateja walitakiwa kuweka na kupokea pesa kwenye akaunti ya Tigo Pesa kutoka kwa wakala wa Tigo Pesa, benki au mitandao mingine na moja kwa moja unakuwa kwenye nafasi ya kushinda.Tunawashukuru wateja wetu kwa kushiriki kwenye kampeni hii na tunawapongeza washindi wote,” alisema.

 

Anna Mkongwa ambaye ameshinda Sh10 milioni alisema “Kwakweli siamini kama nimeshinda, nawashukuru sana Tigo kwa kuleta kampeni hii. “