Msaada wa barakoa, suti za kujilinda na corona wawasili Tanzania

Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu leo Jumatano Machi 25, 2020 ameeleza kuwa Tanzania imepokea msaada wa vifaa tiba vya kupambana na maambukizi ya virusi vya corona.
Vifaa hivyo vimetolewa na mfanyabiashara maarufu wa nchini China, Jack Ma ambavyo vilifika nchini Ethiopia kwa ajili ya kusambaza nchi 54 za Afrika ni barakoa, vifaa vya kupimia na suti za kujilinda na maambukizi.
Ummy kupitia mtandao wa Twitter ameeleza ndege hiyo imefika usiku wa kuamkia leo Jumatano na amemshukuru Ma na serikali ya Ethiopia ambayo ilipokea vifaa hivyo.
Ubalozi wa China nchini Tanzania umesema vifaa vilivyoletwa Tanzania nia barakoa 100,000, vifaa vya upimaji 20,000 na suti za kujilinda 1,000.
Hadi sasa Tanzania ilithibitisha kuwa na  wagonjwa 12 wenye virusi hivyo na Serikali ikieleza hali zao kuendelea vizuri na wengine baada ya vipimo wamekutwa hawana tena.