VIDEO: EAC yatoa ‘maabara zinazotembea’ kwa nchi wanachama kupima virusi vya corona

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC),Balozi Liberat Mfumukeko akizungumza na waandishi wa habari kabla ya kukabidhi maabara zinazotembea kwa nchi wanachama kwaajili ya kukabiliana na magonjwa ya milipuko ukiwemo ugonjwa wa Corona jijini Arusha leo,kulia ni Mkuu wa idara ya Afya ya EAC,Dk Michael Katende.Picha na Filbert Rweyemamu

Muktasari:

  • Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC) leo Jumatano Aprili 15, 2020 imetoa msaada wa maabara zinazotembea kwa nchini wanachama kwa ajili ya kupima virusi vya corona.

Arusha. Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC) leo Jumatano Aprili 15, 2020 imetoa msaada wa maabara zinazotembea kwa nchini wanachama kwa ajili ya kupima virusi vya corona.

Maabara hizo zipo katika magari, Tanzania imepatiwa magari mawili sawa na Kenya na Uganda huku Rwanda, Burundi na Sudan Kusini kila nchi ikipatiwa gari moja.

Lengo la maabara hizo ni kuongeza kasi ya upimaji wa  homa ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona.

Katibu mkuu wa EAC, Balozi Liberati Mfumukeko ametoa taarifa hiyo leo Jumatano Aprili 15, 2020 makao makuu ya jumuiya huyo jijini Arusha na kueleza pia wametoa vifaa kinga kwa watoa huduma

"Maabara moja inatumia  magari mawili kwa ajili ya vifaa mbalimbali  na kukaa maafisa wa afya," amesema

Mkuu wa kitengo cha afya wa EAC, Michael Katende amesema maabara hizo tisa zina thamani ya dola 1.8 milioni ambazo ni zaidi ya Sh3.6  bilioni.

Amesema maabara hizo licha ya kupima corona kwa wakati pia zitaweza kupima magonjwa mengine ya mlipuko kama Ebola.

Magari hayo  yameondoka leo makao makuu ya jumuiya hiyo kwenda  katika nchi wanachama na yatapokelewa mipakani na serikali husika.