Majaliwa: Wanaotaka ubunge, udiwani wasubiri Juni 2020

Muktasari:

Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewataka wanachama wa CCM wanaotaka ubunge na udiwani kusubiri hadi Juni 2020.

Kigoma. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewataka wanachama wa CCM wanaotaka ubunge na udiwani kusubiri hadi Juni 2020.

Amesema kuanzia Juni, waliopo sasa watakuwa wamemaliza muda wao.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Februari 21, 2020 katika kikao cha halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Kigoma.

Amesema wabunge na madiwani wanatakiwa kuachwa watekeleze na kukamilisha ahadi zao walizozitoa wakati wakiomba kura kwa wananchi.

"Wabunge na madiwani wasivamiwe na mtu yeyote waachwe wafanye kazi yao mpaka tarehe ya mwisho chama kitakapo tangaza.”

"Mapungufu kwenye chama ni yetu na usitoke hapa leo na kuingia kwa mtu na kuanza kuimba upungufu ya mbunge au diwani aliyeko madarakani,  kwa kufanya hivyo tutakuwa tunajiua na kujimaliza wenyewe,” amesema Majaliwa.

Amesema lazima viongozi waheshimu watu wao waliowapa dhamana.

Majaliwa amewasili mkoani Kigoma kwa ziara ya siku mbili.