Makonda amwalika Majaliwa kuhudhuria Fiesta Dar

Muktasari:

Kilele cha Tamasha la Fiesta litafanyika Desemba 8, 2019 ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amemwalika Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam nchini Tanzania, Paul Makonda amemueleza Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Kassim Majaliwa akihitaji kupata burudani aje jijini Dar es Salaam kwa kuwa limesheheni kila aina ya burudani.

Makonda ameyasema hayo wakati wa kongamano la sanaa la Mwalimu Nyerere linalofanyika leo Ijumaa Novemba 15, 2019 jijini Dar es Salaam.

Makonda ametumia fursa hiyo pia kumualika Majaliwa katika tamasha la Fiesta linalotarajiwa kufanyika Desemba 8, 2019 katika Uwanja wa Uhuru.

“Mheshimiwa waziri Mkuu, naomba nikutaarifu kuwa Dar es Salaam ni mkoa wa burudani, ukichoka stress za Dodoma njoo Dar ule bata,” amesema Makonda

“Huku kuna magiant watatu, wa kwanza ni Wasafi limeshafanyika (Novemba 9, 2019), linafuata Fiesta halafu muziki mnene hawa bado hawajapanga tarehe,” amesema

”Nitumie fursa hii kukukaribisha Desemba 8 pale uwanja wa Uhuru uje uwaone vijana wako wakifanya kazi kubwa ya kuwapa burudani Watanzania,” amesema Makonda