Mobisol kutoa zawadi ya betri, paneli watakaonunua sola

Muktasari:

  • Kampuni ya uuzaji vifaa vya umemejua, Mobisol imetangaza unafuu huo ili kuwarahisishia wateja wake kufunga mfumo utakaowapa umeme kwa gharama nafuu hivyo kuboresha maisha wa namna moja au nyingine.

Dar es Salaam. Katika kuhamasisha matumizi ya umemejua, kampuni ya Mobisol imetangaza kuanza kutoa betri na paneli bure kwa wateja wake wapya.

Utaratibu huo umetangazwa leo Alhamisi Agosti 22, 2019 jijini Dar es Salaam na meneja mauzo na masoko wa Mobisol kanda ya Pwani, Wesley Muyenze alipokuwa anaeleza mafanikio na mikakati ya kampuni hiyo.

"Kutokana  na  kuongezeka  kwa  idadi ya wateja  wetu, tumeamua kutoa zawadi, mteja akinunua mtambo wa watts 40 anapata betri na paneli bure. Niwaombe  Watanzania  wanahitaji sola kufika dukani kwetu  ili kujipatia zawadi hizo," amesema.

Umemejua ni miongoni mwa vyanzo makini vya umeme vinavyotumika maeneo mengi duniani huku ukichangia kwa kiasi kwenye gridi ya Taifa nchini. Kwa sasa, Tanzania inazalisha zaidi ya megawati 1,600 kutoka vyanzo mbalimbali na miradi mingine ikiendelea kutekelezwa ukiwamo Bwawa la Julius Nyerere huko Rufiji.

Tangu waanze kuuza bidhaa zao nchini, Muyenze amesema wameshanufaisha wateja 100,000 hivyo kuwaunganisha zaidi ya watu 500,000 kwenye nishati hiyo ikicangiwa na kuongezeka kwa uelewa.

Amesema mkakati wa Serikali ya Tanzania kufikia uchumi wa viwanda mwaka 2025 unahitaji umeme wa uhakika kwa wananchi waliopo maeneo tofauti ili washiriki kikamilifu kwenye safari hiyo na umemejua ni miongoni mwa vyanzo vinavyopaswa kupewa kipaumbele.

Kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanaachana na vyanzo vinavyochafua mazingira kama kuni na mkaa, Muyenze amesema watashirikiana na Serikali inayotumia vyanzo vilivyozoleka kupeleka umeme hata kwa wananchi wa vijijini.