Rais Magufuli amwaga ajira 1,000 za madaktari

Muktasari:

Rais wa Tanzania, John Magufuli ametoa kibali cha kuajiri madaktari wapya 1,000 ili kutatua changamoto ya uhaba wa wataalam hao wa afya nchini.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli ametoa kibali cha kuajiri madaktari wapya 1,000 ili kutatua changamoto ya uhaba wa wataalam hao wa afya nchini.

Kiongozi mkuu huyo wa nchi ametoa kibali hicho leo Alhamisi Februari 20, 2020 katika mkutano wa madaktari pamoja na watumishi wa sekta ya afya uliofanyika katika ukumbi wa kimataifa wa mikutano wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.

“Ninafahamu kuna madaktari karibia 2,700 hawajaajiriwa, nitalifanyia kazi. Nafikiri tunaweza tukaanza polepole hata tukachukua 1,000 eti Waziri wa Utumishi (George Mkuchika) hatuwezi kuajiri hata 1000,” amehoji Rais Magufuli.

“Hela si zipo kidogo? Basi tuajiri 1,000 madaktari, tuanze na 1,000 mambo yakiwa mazuri tena tunaajiri wengine kwa sababu tunahitaji madaktari mpaka vijijini.”

Amesema madaktari hao wanatakiwa kuajiriwa ile kupata uzoefu wa vifaa vipya vinavyoingia nchini, “hawa 1,000 madaktari waajiriwe wakapate experience (uzoefu) ya mavifaa haya yanayokuja na wagawanywe vizuri katika mikoa yote.”