Rais Ufaransa aomba radhi wimbo 'feki' wa taifa kabla ya mechi ya Euro 2020

Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa

Muktasari:

Waendeshaji shughuli za uwanjani walitumia wimbo wa Taifa wa Andorra kabla ya mechi baina ya Ufaransa na Albania na baadaye mratibu kuwaomba radhi mashabiki wa Armenia

Tirana, Albania. Waziri Mkuu wa Albania, Edi Rama jumapili alisema kuwa Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa aliomba radhi kwa kuchezwa wimbo usio sahihi wa taifa kabla ya mechi ya soka baina ya nchi hizo iliyoiisha kwa Ufaransa kushinda kwa mabao 4-2.
Mechi hiyo ni ya awali ya michuano ya kuwania tiketi ya kucheza fainali za Euro 2020.
Mechi hiyo iliyofanyika kwenye uwanja wa Stade de France Jumamosi iliyopita, ilichelewa kuanza baada ya kuchezwa wimbo wa taifa wa Andorra kabla ya mtanmgazaji uwanjani kuomba radhi kwa "mashabiki wa Armenia" baada ya wimbo sahihi kuchezwa.
"Rais Macron aliwasilisha ujumbe wake wa kuomba radhi kwa kashfa hiyo inayolihusu Shirikisho la Soka la Ufaransa kuhusu wimbo wetu wa taifa," aliandika waziri huyo mkuu katika akaunti yake ya Twitter.
"Rais wa Ufaransa amechukuliwa kosa hilo kuwa halikubaliki na amefurahia jinsi wachezaji wetu walivyolipokea," alisema.
Ofisi ya Rais Macron ilithibitisha kitendo hicho cha kuomba radhi ilipoulizwa na AFP.
Kocha wa Ufaransa, Didier Deschamps pia aliomba radhi kw amwenzake wa Albania, Edoardo Reja, kutokana na kosa hilo.
Ufaransa, iliyo kileleni mwa Kundi H, leo inacheza na Andorra katika mechi nyingine ya michuano ya awali ya Euro 2020 wakati Albania inavaana na Iceland.