VIDEO: Sumaye aeleza sababu ya kuhama CCM, kujiunga Chadema

Muktasari:

  • Waziri mkuu mstaafu wa Tanzania, Frederick Sumaye amesema uamuzi wake wa kuhama CCM na kujiunga na Chadema ulikuwa na lengo la kuimarisha upinzani

Dar es Salaam. Waziri mkuu mstaafu wa Tanzania, Frederick Sumaye amesema uamuzi wake wa kuhama CCM na kujiunga na Chadema ulikuwa na lengo la kuimarisha upinzani.

Akizungumza leo Jumatano Novemba 4, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari, Sumaye amesema kujiunga upinzani si jambo rahisi, kwamba alikuwa akiandamwa na Dola pamoja na familia yake.

Sumaye aliyekuwa waziri mkuu mwaka 1995 hadi 2005 amesema hayo takribani siku nne tangu alipopigiwa kura 48 za hapana kati ya 76 katika uchaguzi wa uenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani.

Sumaye amesema alikusudia kuhamia upinzani Agosti 22, 2015 kuuimarisha na hatua hiyo inaifanya  CCM isilale usingizi,” leo  CCM na serikali yake hawalali usingizi wanazunguka nchi nzima kufanya kazi."

"Nimekuja upinzani kwa lengo la awali la kuimarisha upinzani wa dhati na kuchukua dola. Mimi sikuja Chadema kutafuta vyeo, wakati nahamia upinzani tayari vyama vilikuwa vimepanga wagombea wa tayari."

Katika mkutano huo na wanahabari, Sumaye ameongozana na mratibu wa Chadema Kanda ya Pwani, Casmiri Mabina aliyemkaribisha Sumaye kuzungumza na waandishi wa habari.