Upelelezi kesi anayedaiwa kumuua mkewe, kumchoma kwa mkaa wakamilika

Muktasari:

  • Upande wa mashtaka katika esi ya mauaji inayomkabili Mfanyabiashara Hamis Said (38) umedai upelelezi wa shauri hilo umekamilika na jalada la shauri hilo lipo kwenye hatua ya uchapaji ili kulipeleka Mahakama Kuu ya Tanzania.

Dar es Salaam. Upande wa mashtaka katika kesi ya mauaji inayomkabili Mfanyabiashara Hamis Said (38) umedai upelelezi wa shauri hilo umekamilika na jalada la shauri hilo lipo kwenye hatua ya uchapaji.

Wakili  wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon amedai hayo leo Jumatatu Oktoba 21, 2019 mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam kuwa shauri lilikuja kwa ajili ya kutajwa na upelelezi umekamilika.

Simon amedai jalada la shauri hilo lipo kwenye hatua ya uchapaji kwa ajili ya maandalizi ili lipelekwe Mahakama Kuu ya Tanzania hivyo ameiomba mahakama hiyo ihairishe kesi hiyo.

 

Hakimu Mkazi Mkuu, Salum Ally aliahirisha shauri hilo hadi Novemba 4, 2019.

Katika kesi ya msingi mshtakiwa anakabiliwa na kosa moja la mauaji ambapo anadaiwa  Mei 15, 2019 katika oneo la Geza Ulole Kigamboni Dar es Salaam alimuua mtu anayeitwa Naomi Marajani kisha kumchoma kwa mkaa na mabaki kwenda kuyazika Mkuranga mkoani Pwani.