Katibu Basata akumbushia ugomvi wa Diamond, Rayvanny

Muktasari:

  • Mwanamuziki Rayvanny tayari amewasili nchini kutoka Kenya ambapo alienda kwenye hafla ya utolewaji tuzo za East Africa Arts Entertainment Awards 2024 (EAEA) ambapo ameondoka na tuzo tano.

Dar es Salaam. Mwanamuziki Rayvanny tayari amewasili nchini kutoka Kenya ambapo alienda kwenye hafla ya utolewaji tuzo za East Africa Arts Entertainment Awards 2024 (EAEA) ambapo ameondoka na tuzo tano.

Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa Dkt. Kedmon Mapana, akiwa katika mapokezi ya msanii huyo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere amesema kuwa alipoingia kazini mwaka 2022 kazi ya kwanza aliyokabidhiwa ni kutatua kesi ya Rayvanny na Diamond

"Tunampongeza sana, watu wengi hawafahamu Rayvanny mimi ni kijana wangu, nilipoingia kazini Julai 12, 2022, kazi ya kwanza niliyokabidhiwa na mheshimiwa waziri wa wakati huo ni kumaliza kesi ya Diamond na Rayvanny, hiyo ndiyo ilikuwa kazi yangu ya kwanza Basata kwa hiyo lazima niikumbuke lakini nashukuru sana Mungu kwamba nilipambana ile kazi iliisha vizuri na vijana wangu walipatana na wakarekdi ngoma," amesema Mapana.

Katika tuzo hizo ambazo Rayvanny amerudi nazo nchini ni tuzo ya Msanii Bora wa Kiume (East Africa), Album/EP bora (East Africa), Mwandishi bora (East Africa), Best lovers’ choice single (East Africa), Best inspirational single (East Africa).

Aidha kwa upande wake Rayvanny akizungumza na waandishi wa habari alipowasili nchini amegusia suala la Harmonize na Diamond kupatana na kuishi kwa amani.

"Mimi ni mtu ninayependa kuweka sana amani pasiwe na ugomvi na vita kama ambavyo mimi nimetoka Wasafi changamoto zilikuwa nyingi lakini tumeweza kuitunza amani na maisha mengine yanaendelea sababu mtu mwingine anajua labda zikishatoka hela unanuna lakini mwisho tunafanya kazi tunafanya biashara familia lazima iendelee pia mimi nilikuwa na kila sababu ya kusema kwamba tunaweza kugombana lakini tuliweza kuitunza amani kwa hiyo nikamwambia pia sioni kama kuna faida yoyote ya kuendelea kugombana nafikiri Harmonize ameongea sana na Diamond kuwa maisha mengine yaendelee". Amesema.

Hata hivyo, kuhusiana na baadhi ya watu wanaodai kuwa kupatana kwa wasanii hao kunaweza kupunguza ushindani wa kimuziki Rayvanny amesema ushindani wa gemu hauwezi kupungua kwani kila mmoja ataendelea kutoa ngoma zake.

Aidha Vanny Boy alimalizia kwa kuzungumzia wimbo wake mpya uitwao 'Hongera' ambao wengi wameuhusisha na ujauzito wa aliyekuwa mpenzi wake Paula Kajala ambaye kwa sasa anatarajia kupata mtoto na mwanamuziki Marioo. Kutokana na hilo Vanny amesema wazo la wimbo huo alipata akiwa kwenye ndege baada ya kumuona mjamzito akiwa anapatiwa huduma ndani ya usafiri huo.

"Siku nilikuwa nipo kwenye ndege kuna mama mmoja alifika alikuwa anapewa huduma kwa kuwa ni mjamzito nikawaza wamama wanapitia changamoto nyingi sana mpaka wanatuzaa sisi kwa sababu kuna wengine wanapenda ujana kwenda klabu lakini hadi mwanamke anapotulia na kukitunza kiumbe miezi tisa siyo kitu kidogo na mama zetu ndiyo wanazaa mashujaa, madaktari nikasema kwa nini nisifanye kitu kupongeza wamama, kwa hiyo nimedediketi kwa wanawake wote wenye ujauzito na waliojifungua. Marioo na Paula wanatarajia mtoto nawapongeza kwa hiyo Paula naye ni mjamzito kwa hiyo pia nina mdediketi". Amesema

Hata hivyo, wasanii wa Tanzania walionyakua tuzo hizo ni Lizer Classic - Best Sound Engineer (East Africa), Mr LG - Best Breakthrough Beat/Hit-Maker (East Africa), Wcb Wasafi - Record Label Of The Year (East Africa), Rayvanny – Best songwriter/lyricist (East Africa), Rayvanny - Best lovers’ choice single (East Africa), Dj Joozey - Best Breakthrough DJ/VJ (East Africa), Dayoo Ft. Rayvanny - "Mwaka Huu" - Best inspirational single (East Africa).

Harmonize Single Again - Overall Hit Single Of The Year (East Africa), Diamond Platnumz - Overall Hit-Maker Artist Of The Year (East Africa), Rayvanny - Best male artist (East Africa), Rayvanny - Best studio album/EP (East Africa), S2kizzy - Overall Hit-Maker Producer Of The Year (East Africa), Jux Ft Diamond Platnumz "Enjoy" - Collaboration Of The Year (East Africa).