Serikali yaahidi kurekebisha kodi, ushuru

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Dk Ashatu Kijaji.

Dar es Salaam. Wakati wafanyabiashara wa bidhaa za misitu wakidai kodi, ushuru, ada na tozo wanazotakiwa kulipa zinaweza kuwaondoa kwenye biashara hiyo, Serikali imeahidi kurekebisha suala hilo ifikapo mwaka wa fedha wa 2023/24.

Akizungumza jana kwenye baraza la saba la biashara Mkoa wa Njombe, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Dk Ashatu Kijaji alisema Wizara ya Fedha na Mipango itaitisha mkutano wa wadau unaotarajiwa kufanyika wiki ijayo ili kutafuta suluhu ya kudumu.

“Suala la kodi ni la kisheria, siwezi kuja kutengua kwa agizo tu, taratibu za kisheria lazima zifuatwe, hivyo mwenzangu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba ameitisha kikao cha wadau Jumatano ya Januari 11,” alisema Dk Kijaji.

Pia, alisema wafanyabiashara na wadau wengine wa uchumi nchini watawasilisha malalamiko yao kuhusiana na kodi; na Serikali itayafanyia kazi na mabadiliko yoyote yatajumuishwa katika muswada ujao wa fedha.

“Tunafanya hivyo kwa nia moja na Rais wetu mpendwa, Samia Suluhu Hassan ambaye ameamua kuimarisha sekta binafsi kwa kuwa ndiyo injini ya uchumi wa nchi. Tusiwe kikwazo kwa sekta binafsi, tunaihitaji kwa uchumi.”

Alisema taasisi hizo zimekadiria kinyume chake kwa Tanzania ambayo ni mojawapo ya nchi zinazokua kwa kasi kiuchumi barani Afrika na utawala wa Rais Samia umepanga kurekodi ukuaji wa angalau asilimia 6.2 kwa mwaka.

Kwa mujibu wa Tathmini ya Hali ya Uchumi wa Tanzania ya mwaka 2022, kutokana na kuimarika kwa utendaji katika utalii, kufunguliwa tena kwa njia za biashara na kuharakishwa kwa utoaji wa chanjo, pato la Taifa (GDP) linatarajiwa kukua kwa asilimia 5.6 mwaka huu.

“Ili kufanya hili kuwa kweli, Serikali inafanya kazi kwa bidii kurekebisha sheria mbalimbali zinazohusiana na kodi ambazo zitaweka mazingira mazuri ya biashara na mkutano wa wiki ijayo ni sehemu ya mpango huu,” alisema Dk Kijaji.

Pia, alisema kuna haja ya wafanyabiashara wa Tanzania kutumia masoko yanayoweza kutoa upendeleo wa kibiashara kama vile Afrika Mashariki, inayojumuisha nchi saba zenye watu milioni 174 na pato la Taifa la takriban Dola 163.4 bilioni za Marekani.

Mbali na soko la EAC, aliitaja pia Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (Sadc) inayojumuisha nchi wanachama 16 zenye watu milioni 344 na pato la Dola bilioni 720 za Marekani.

Dk Kijaji alisema wafanyabiashara wa Tanzania wasikose fursa iliyotolewa na Eneo Huru la Biashara la Bara la Afrika (AfCFTA), ambalo ni soko la bara zima linalojumuisha nchi 55 zenye watu bilioni 1.3 na pato la Taifa la Dola 3.4 trilioni za Marekani kwa pamoja.

“Tuchangamkie fursa hii iliyotolewa na AfCFTA, kwa kweli; Tanzania ni miongoni mwa nchi saba zinazoshiriki katika majaribio ya biashara ya soko, nchi nyingine ni pamoja na Cameroon, Misri, Ghana, Kenya, Mauritius na Rwanda,” alisema Dk Kijaji.

Masoko mengine ambayo biashara ya ndani inapaswa kufikiria, alisema: “Marekani imeongeza Sheria ya Ukuaji na Fursa Afrika (Agoa) - makubaliano yanatoa ufikaji bila ushuru kwenye soko la Marekani kwa mataifa yanayostahiki ya Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ambayo Tanzania ni sehemu yake.”

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Antony Mtaka alisema kuna haja ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na vyombo vingine vyenye jukumu la kukusanya kodi, kutumia busara na weledi katika kutekeleza jukumu hilo.

“Kutisha watu au kutumia jina la Rais kushinikiza wafanyabiashara walipe kodi ni kitendo kisichoeleweka na jina la Rais halipaswi kutiwa moyo kwa kweli; ni mbinu ya kizamani, kuweni na weledi,” alisema Mtaka.