Mlipuko wa Surua wahofiwa katika nchi za Sudan

Wanawake na watoto wamekusanyika katika jengo kwenye kambi ya wakimbizi wa ndani huko al-Suwar, yapata kilomita 15 kaskazini mwa Wad Madani, Sudan. Picha na AFP

Muktasari:

  • Mashirika ya afya katika Jimbo la White Nile lililopo mpakani mwa nchi za Sudan na Sudan kusini, yamesema takriban watoto 13 wamefariki katika muda wa wiki moja iliyopita kufuatia mlipuko unaodhani kuwa ni wa ugonjwa wa surua.

Sudan Kusini. Mashirika ya afya katika Jimbo la White Nile lililopo mpakani mwa nchi za Sudan na Sudan kusini, yamesema takriban watoto 13 wamefariki katika muda wa wiki moja iliyopita kufuatia mlipuko unaodhani kuwa ni wa ugonjwa wa surua.

Maafisa wa Shirika la Kimataifa la Matibabu (MSF) wamesema bado wana wasiwasi kuhusu ongezeko la matukio yanayo husishwa na ugonjwa huo na hasa miongoni mwa watoto katika jimbo hilo.

Akizungumza na kituo cha habari ‘VOA’ Mitchell Sangma, mshauri wa afya wa MSF, amesema shirika lake limeripoti zaidi ya visa 200 vinavyoshukiwa kuwa vya surua miongoni mwa watoto mwezi uliopita, ambapo kati ya idadi hiyo, 72 walilazwa hospitalini na 13 walifariki dunia.

"Pia tunaona kuongezeka kwa idadi ya watoto wanaodhaniwa kuwa na surua katika miradi yetu mingine kama vile katika jimbo la Blue Nile nchini Sudan. Na huko Renk, upande mwingine wa mpaka wa Sudan Kusini, pia tunaona ongezeko la matukio ya surua katika wodi zetu….Kwa hiyo, hali ya watu wanaokimbia migogoro inazidisha wasiwasi sana,” amesema.

Afisa huyo wa MSF anasema mzozo uliodumu kwa takriban miezi mitatu nchini Sudan kati ya jeshi na kundi pinzani la wanamgambo umezua hitaji kubwa la matibabu na shinikizo kubwa kwa vituo vya afya kote nchini.

Sangma amesema MSF na mashirika mengine ya misaada yana wasiwasi kuhusu kuporomoka kwa mfumo wa afya katika nchi hizo mbili ambapo apo awali zilikuwa ni taifa moja.

Mshauri huyo wa amebainisha kuwa msimu wa mvua unapokaribia, kuna uwezekano mkubwa wa milipuko ya magonjwa miongoni mwa mamilioni ya watu waliokimbia makazi yao kutokana na vita.

Shirika hilo linasema kuna haja ya kuongeza huduma kama vile chanjo, msaada wa lishe, makazi, maji na usafi wa mazingira.