Mwanamke ajifungua akiwa amefunikwa na kifusi

Mtoto huyo anayedaiwa kuwa na siku moja akiwa kwenye mashine maalumu katika hospitali kwenye mji wa Afrin.

Da es Salaam. Mtoto mchanga anayekadiriwa wa siku moja, ameokolewa kwenye kifusi baada ya mama yake kufukiwa kwenye moja ya jengo lililoporomoka pamoja na wanafamilia wengine saba kutokana na tetemeko la ardhi lililotokea juzi Jumatatu Uturuki na Syria na kusababisha vifo vya watu takribani 9,000 hadi sasa.

 Kikosi cha uokoaji kilifanikiwa kumnasua mtoto huyo jana Jumanne Februari 07, 2023 kisha kumuwahishwa Hospitali katika mji wa Afrin nchini Syria.

Shirika la Habari la AFP limeelezwa kuwa mtoto huyo alikutwa bado kitovu chake kimeungana na mama yake ambaye tayari alikuwa ameshafariki dunia.

Taarifa zinaeleza kuwa huenda mama huyo alifariki muda mfupi baada ya kujifungua akiwa kwenye kifusi baada ya kuporomokewa na ghorofa alilokuwa akiishi na familia yake.

Video iliyosambaa mitandaoni imemuonyesha muokoaji akiwa amemshika mtoto huyo aliyekuwa ametapakaa vumbi.

Hata hivyo muda mfupi mtoto huyo aliwahishwa hospitalini na kupatiwa matibabu pamoja na kuhifadhiwa kwenye kifaa maalumu. Picha zilizosamba mtandaoni zilionyesha mtoto huyo akiwa na michubuko sehemu za mgongoni.

Miili mingine iliyopatikana katika eneo hilo ni pamoja na baba yake aliyetambulika kwa jina la Abdullah na mama yake aliyetambuliwa kwa jina la Afraa, na wanafamilia wengine watano.

Shuhuda wa tukio hilo aliyenusurika alisema “Abdullah ni binamu yangu na nimemuoa dada yake.”

Daktari Hani Maarouf anayemhudumia mtoto huyo alisema, kichanga huyo anaendelea vizuri.

“Vidole vyake vilikuwa vimejikunja kwa sababu ya kupigwa na baridi na mwili wake una majeraha kiasi. Ameletwa hapa akiwa kwenye hali mbaya na alikuwa akipata shida ya kupumua kutokana na baridi kali, tulifanya juhudi kumuweka kwenye mashine ya joto,” amesema.

Kwa mujibu wa kikosi cha uokoaji kimesema kwamba zaidi ya majengo 210 yameanguka na mengine 520 yameharibika kutokana na tetemeko hilo la kipimo cha 7.8.

Mnamo 1999, watu 17,000 walifariki kutokana na tetemeko la ardhi la kipimo cha 7.4 na kurekodiwa kuwa janga baya zaidi kuwahi kutokea katika nchi ya Uturuki ambayo ni majirani na Syria.