17 wachukua fomu kumrithi Ole Nasha Ngorongoro

17 wachukua fomu kumrithi Ole Nasha Ngorongoro

Muktasari:

  • Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Ngorongoro unafanyika kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, William Ole Nasha aliyefariki dunia Septemba 27, mwaka huu kwa ugonjwa moyo.

Arusha. Baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kutangaza kuwa Jimbo la Ngorongoro liko wazi, tayari wagombea 17 watatu wakiwa wanawake wamejitokeza kuchukuwa fomu kuwania uteuzi wa kugombea ubunge katika Jimbo la Ngorongoro mkoani Arusha, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Uchaguzi huo mdogo unafanyika kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, William Ole Nasha aliyefariki ghafla akiwa nyumbani kwake Medeli jijini Dodoma, Septemba 27, mwaka huu.

Kwa mujibu wa ratiba ya NEC, uchaguzi huo mdogo umepangwa kufanyika Desemba 11, 2021.

Akizungumza uchukuaji fomu, Katibu wa CCM Wilaya ya Ngorongoro, Amos Shimba aliwataja makada waliochukua fomu mpaka sasa na kurejesha kuwa ni mwenyekiti wa zamani wa halmashauri hiyo, Elias Ngorisa na Mkurugenzi Mkuu Taasisi ya kudhibiti ubora wa mbegu (TOSCI), Patrick Ngwediagi.

Wengine ni Wakili Daud Haraka na Patrick Girigo na mtoto wa mbunge wa zamani wa jimbo hilo, William Telele.
Wengine ni Mkurugenzi wa Shirika la Jamii ya wafugaji (TPCF), Joseph Parsambei, Leyani Sabore, Moloimet Olarwas, Mhadhiri Mwandamizi Chuo Kikuu cha Makumura, Dk Elifuraha Lalkaita na Mhadhiri Chuo cha Wanyamapori Mwika, Dk Kakoi Melubo.

Katika kinyang'anyiro hicho kuna makada watatu waliojitosa kuchukua fomu ambao ni Elinora Oldaraseroa, Mesha Pius na Rose Njiro.


"Hadi sasa tuna wagombea 17 ambao tayari wamechukua fomu na hadi saa 10 jioni tutatoa orodha wote waliochukuwa na kurejesha fomu," amesema.


Hata hivyo, Katibu huyo amewaonya waliochukuwa fomu kuacha kufanya mambo yanayokiuka kanuni na taratibu za Chama ikiwemo kufanya kampeni na kwamba, atakayebainika atakuwa amepoteza sifa.


"Baada ya zoezi hili kukamilika kesho tutapiga kura za maoni na baadaye kesho kutwa vikao vya kupitia majina vitaanza ngazi ya wilaya baadaye Mkoa kisha Taifa," amesema.