‘Aua’ mke kisha kujinyonga kisa mapenzi


Muktasari:

  • Watu watatu wamefariki dunia katika matukio mawili tofauti mkoani Songwe.

Songwe. Watu watatu wamefariki dunia katika matukio mawili tofauti, likiwamo la mwanaume kumuua mkewe kisha naye kujinyonga mkoani Songwe.

Kamanda wa Polisi Mkoani Songwe, Theopista Mallya amesema tukio la kwanza limetokea Kata ya Mkulwe wilayani Momba ambako mwanaume ambaye jina lake bado halijafahamika amemuua mkewe kwa kumchoma kisu na hatimaye naye kujinyonga.
"Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia jana na kuwa chanzo cha mauaji hayo inasadikiwa kuwa ni wivu wa kimapenzi" amesema Kamanda Mallya
Katika tukio lingine mwili wa msichana anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka kati ya 15 na 19 umekutwa akiwa ameuawa katika Mtaa wa Shule katika Mji mdogo wa Mlowo wilayani Mbozi muda wa saa tatu asubuhi.
Kamanda Mallya amesema uchunguzi kuhusiana na tukio hilo unaendelea na kuwa mwili wa Marehemu huyo umehifadhiwa katika Hospitali ya Serikali ya Wilaya Mbozi (Vwawa).