Bunge lataka ufumbuzi msongamano wa wafungwa, mahabusu

Muktasari:
- Kamati ya Bunge ya Ukimwi na dawa za kulevya imeitaka ofisi wa waziri mkuu kutafuta ufumbuzi wa msongamano wa wafungwa na mahabusu kwenye magereza nchini ili kuepuka kusambaa kwa magonjwa.
Dodoma. Kamati ya Bunge ya Ukimwi na dawa za kulevya imeitaka ofisi wa waziri mkuu kutafuta ufumbuzi wa msongamano wa wafungwa na mahabusu kwenye magereza nchini ili kuepuka kusambaa kwa magonjwa.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Fatma Toufiq ameyasema hayo bungeni mjini Dodoma leo Jumanne Aprili 13, 2021 wakati akiwasilisha maoni ya kamati kuhusu makadirio, mapato na matumizi ya fedha ya ofisi ya waziri mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2021/22.
Amesema magereza nyingi zina msongamano hali inayosababisha kukosekana kwa mzunguko wa kutosha wa hewa kwa wafungwa na mahabusu.
“Mazingira haya yanachochea maambukizi ya ugonjwa wa kifua kikuu kwa haraka. Kamati ilibaini
kuwa ili kukabiliana na kuenea kwa ugonjwa wa kifua kikuu hatua za awali za upimaji na kuanzishiwa dawa kwa wanaokutwa na kifua kikuu ni njia ya inayotumika katika mapambano dhidi ya kifua kikuu,” amesema.
Amesema hali ya msongamano magerezani inaweza kupatiwa ufumbuzi chini ya uratibu unaofanywa na ofisi ya waziri mkuu.