Abiria 400 wahesabiwa wakisafiri ndani ya meli Ziwa Victoria
Muktasari:
- Sensa ya Watu na Makazi imeanza Jumanne Agosti 23, 2022 na itaendelea kufanyika ndani ya siku saba
Mwanza. Abiria zaidi ya 400 waliokuwa wakisafiri kutoka bandari ya Bukoba mkoani Kagera kwenda Mwanza wakitumia meli ya New Mv Victoria ‘Hapa Kazi Tu’ wamehesabiwa wakiwa safarini katikati ya maji ya Ziwa Victoria.
Akitoa taarifa kwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Adam Malima Agosti 23, 2022 alipokuwa akitembelea Kata mbalimbali za mkoa huo kujionea namna Sensa inavyofanyika, Mkufunzi wa Sensa Wilaya ya Nyamagana, Bertha Ntanwa amesema kuhesabiwa kwa abiria hao ni utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kuhakikisha watu wote wakiwemo wasafiri wanahesabiwa.
“Tulikuwa makarani wawili, ilivyofika Saa 6:02 usiku tulianza kufanya mahojiano. Tumedodosa abiria zaidi ya 400, wahudumu na nahodha,”amesema
Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Selemani Sekiete amesema wamefikia watu waliolala katika hoteli 78 na lodge 314 zinazopatikana Wilaya ya Nyamagana ili kuwapa haki yao ya kuhesabiwa.
Akizungumza na wananchi eneo la Mirongo jijini Mwanza, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Adam Malima amewatoa hofu wakazi wa mkoa huo ambao hawajafikiwa na makarani wa Sensa kuwa itaendeleo ndani ya siku saba.
“Leo tumeanza vizuri, matarajio yangu ambao hawatohesabiwa leo watahesabiwa kesho. Tutatoa taarifa na matangazo kwenye yale maeneo ambayo hayajafikiwa ili wafahamu na kujiandaa kuhesabiwa siku inayofuata,”amesema Malima
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Amina Makilagi amesema wamehesabu watu waliokuwa kwenye hoteli za jijini Mwanza, kwenye meli iliyotoka Kagera kuja Mwanza pamoja na
Watu wanaolala vibarazani wakiwemo watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu.
“Tulifanya Sensa kwa watoto wa mitaani ambao tuliwaandalia mkakati maalum wa kuwafata kule walipo na tuliwahesabu wote katika mitaa na vijiwe vyao,”amesema Makilagi