Anayedaiwa kummwagia Tariq tindikali akamatwa

Muktasari:

Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro linamshikilia mtu mmoja kwa tuhuma za kummwagia mkazi wa Manispaa ya Moshi, Tariq Awadhi (31) tindikali.

Moshi. Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro linamshikilia mtu mmoja kwa tuhuma za kummwagia mkazi wa Manispaa ya Moshi, Tariq Awadhi (31) tindikali.

Tariq alimwagiwa tindikali usoni na mikononi siku 45 zilizopita na kulazwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC.

Akizungumzia tukio hilo leo Aprili 19, 2022 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa amesema wanamshikilia mtuhumiwa huyo na tayari upelelezi umeshakamilika juu ya tukio hilo.

Kamanda Maigwa ambaye hakutaka kutaja jina la mtuhumiwa huyo kwasababu za kiuchunguzi na usalama amesema tayari wameshaandaa jalada la mashtaka na wameshalikabidhi kwa mwanasheria wa Serikali kwa hatua zaidi.

"Ni kweli tumemkamata mtuhumiwa na amekiri mwenyewe kutenda kosa hilo na tayari tumeshamfungulia jalada la mashtaka na tayari tumeshapeleka kwa mwanasheria mkuu wa serikali kwa ajili ya hatua za kisheria zaidi,"amesema na kuongeza

"Tayari upelelezi umeshakamilika na muda wowote atafikishwa mahakamani,"amesema Kamanda Maigwa

Tariq alifikwa na madhila hayo Machi 5 mwaka huu wakati akitoka nyumbani kwake Shant town kwenda sehemu ya kwenda kula chakula cha jioni