Asakwa na polisi akidaiwa kumbaka mtoto wa miaka mitano, kumuua

Asakwa na polisi akidaiwa kumbaka mtoto wa miaka mitano, kumuua

Muktasari:

  • Mkazi wa kijiji cha Mutuka wilayani Babati Mkoa wa Manyara, Emmanuel Naasi (30) anasakwa na polisi akituhumiwa kumbaka na kumuua mtoto wa kaka yake mwenye umri wa miaka mitano.

Babati. Mkazi wa kijiji cha Mutuka wilayani Babati Mkoa wa Manyara, Emmanuel Naasi (30) anasakwa na polisi akituhumiwa kumbaka na kumuua mtoto wa kaka yake mwenye umri wa miaka mitano.

Akizungumza leo Jumanne Julai 6, 2021 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Merrison Mwakyoma amesema tukio hilo limetokea jana Julai 5, 2021  saa 12 jioni na kwamba Naasi alikutana na mtoto huyo na wenzake wawili wakitoka kuchota maji na kuanza kuwakimbiza.

“Kila mmoja alikimbilia upande wake lakini yeye alimkamata marehemu, alimbaka na kisha alimpiga na kitu kizito usoni na mtoto huyo akafariki dunia papo hapo,” amesema kamanda Mwakyoma akibainisha kuwa baada ya kitendo hicho, mtuhumiwa huyo alikimbia.

Amesema watoto wawili waliokuwa na marehemu ndio waliokwenda kutoa taarifa kijijini na shughuli ya kutafuta mwili ikaanza na kupatikana saa 2 usiku.

“Mwili umehifadhiwa kwenye hospitali ya Mrara ya mji wa Babati na mtuhumiwa anaendelea kutafutwa,” amesisitiza.