Bei ya nyama ya ng'ombe yapanda Mbeya
Ofisa mifugo Bodi ya Nyama Tanzania (TMB) Kanda ya nyanda za juu kusini , Dk Mpoki Alinanuswe akikagua ubora wa nyama katika moja ya bucha katika kata ya Isyesye jijini Mbeya leo Alhamisi June 15, 2023. Picha na Hawa Mathias
Muktasari:
- Bodi ya Nyama Tanzania (TMB) Kanda ya nyanda za Juu Kusini imeeleza sababu kubwa ni baadhi ya wafugaji kusitisha kuuza na badala yake kuuza mazao ili kutatua mahitaji muhimu hususan kuwepo kwa maeneo ya malisho msimu huu wa mavuno.
Mbeya. Kufuatia kupanda kwa bei ya nyama katika baadhi ya mabucha jijini Mbeya, Bodi ya Nyama Tanzania (TMB) Kanda ya Nyanda za Juu imeeleza sababu kubwa ni wafugaji kusitisha kuuza,katika msimu huu wa mavuno ikiwepo uhakika wa maeneo ya malisho ya mifugo.
Bei hizo zimepanda tangu Jumanne , June 13,2023 kutoka Sh 8,000 kwa kilo moja mpaka Sh 9,000 na 9,500 katika baadhi ya bucha Jijini hapa hali ambayo imekuwa ni changamoto kwa walaji wa kipato cha chini.
Akizungumza na Mwananchi leo June 15,2023 Ofisa mifugo bodi ya nyama Kanda ,Dk Mpoki Alinanuswe amesema kila mwaka msimu wa mavuno kuna changamoto ya upatikanaji wa ng'ombe kutokana na idadi kubwa ya wafugaji wanapokuwa na mahitaji muhimu ya kifamilia kuuza mazao badala ya mifugo.
“Ukitaka kuangalia katika misimu ya mavuno kunajitokeza changamoto za gharama za nyama kupanda yote hiyo ni sababu ya uhaba wa ng'ombe kutokana na wafugaji kusitisha kuuza mifugo na badala yake kuuza mazao kutatua changamoto za mahitaji muhimu ya kifamilia ”amesema Dk ,Alinanuswe.
Dk ,Alinanuswe amesema kufuatia hali hiyo jana ,Jumatano June 14,2023 wameanza kufanya ukaguzi wa ubora wa nyama ikiwepo matumizi ya vifaa vya kisasa hususan mizani za kupimia kitoweo hicho.
“Mkoa wa Mbeya tuna bucha zaidi ya 450 tutafanya ukaguzi katika maeneo yote kujiridhisha ubora wa nyama ambapo jana June 15,2023 tumekagua bucha 11 katika kata ya Ituha na Isyesye jijini hapa sambamba na kuwasikiliza wauzaji ”amesema.
Amesema kupanda kwa bei ya nyama kunaweza kushusha takwimu za ulaji wa nyama ambapo kitaifa mtu mmoja anapaswa kula kilo 50 kwa Mwaka hivyo kuna kazi kubwa kwa bodi kuendelea kuhamsisha jamii licha ya kuwepo kwa changamoto ya kupanda na kushuka kwa bei.
Mfanyabishara wa bucha ya Nyama , Elieza John amesema kwa kipindi cha mwezi mmoja sasa hali ya upatikanaji wa ng'ombe imekuwa ngumu huku ng'ombe waliokuwa wakinunua 800,000 wanauziwa kati ya Sh 1.2 millioni .
“Kimsingi hali ni mbaya na hata upatikanaji wake umekuwa wa shida kwani wafugaji kwa sasa hawana changamoto kubwa sana za fedha mpaka hapo msimu wa kilimo utakapoanza”amesema.
Naye Mama lishe ,Rehema Manjonde amesema kutokana na bei ya nyama kupanda kutoka Sh 8,000 mpaka Sh 9,000 wamelazimika kupungua kiwango cha ukataji wa vipande vya kitoweo hicho.
“Kwa mfano wali nyama nilikuwa nauza Sh 2,500 lakini sasa nauza Sh 3,000 na tunauza bei hizo kulinda mitaji na wateja wasikimbie”amesema.