DC Arumeru atoa siku saba wananchi kung'oa bangi shambani
Mkuu wa wilaya Arumeru Emmanuela Kaganda akionesha bangi iliyovunwa na kuhifadhiwa kwenye masufuria Kijiji Cha Kisimiri juu.
Arusha. Wananchi wa Kijiji cha kisimiri Juu wilaya ya Arumeru wamepewa siku saba kung'oa miche ya bangi katika mashamba yao baada ya kubainika kuendelea na kilimo hicho licha ya kupigwa marufuku.
Kubainika kwa mashamba hayo katika Kijiji hicho kumetokana na operesheni iliyofanywa na kamati ya ulinzi na usalama katika wilaya hiyo kwa kushirikiana na baadhi ya Wananchi iliyofanyika June 11, 2023 na kufanikiwa kung’oa hekari 60 za zao hilo.
Maagizo hayo yamekuja takriban siku tatu tangu operesheni nyingine iliyofanywa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za kulevya (DCEA) iliyoongozwa na Kamishna Jenerali Aretas Lyimo katika vijiji vya Arumeru ambapo gunia 931 za Bangi zilikamatwa Arumeru.
Katika operesheni hiyo iliyofanyika kijiji cha Lesinoni na maeneo ya jirani pia hekari 953 za bangi ziliteketezwa na ilibainika uwepo wa bangi mbichi gunia 4,975 na watu 16 walikamatwa.
Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Emmanuela Kaganda akizungumza wakati wa operesheni Kijiji Cha Kisimiri ameonya baadhi ya wananchi kuendelea kwa Kilimo hicho na kutoa siku Saba kung'oa bangi mashambani.
"Baada ya siku saba tutafanya opesheni kubwa mashambani na ambao mashamba yao yatakutwa na bangi hatua kali za kisheria zitachukuliwa,"amesema.
Amesema katika operesheni hiyo wamefanikiwa kukamata gunia 10 za bangi kavu, kukusanya mbegu za bangi kg 30 na kuteketeza hekari 60 za mashamba ya bangi mbichi.
Mwenyekiti wa kijiji hicho, Mayani Lukumay ameiomba Serikali kuboresha miundombinu ya barabara kufika kijijini hapo kwani wananchi wanaweza kulima mazao mengi.
"Eneo hili tunaweza kupata mavuno makubwa Kama tukiongeza nguvu katika kilimo cha viazi, njegere,pareto lakini changamoto kubwa ni namna ya kuyafikisha mazao hayo sokoni,"amesema.