Dk Kashilillah achukua fomu ya kuwania uspika

Muktasari:

  • Aliyewahi kuwa Katibu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Dk Thomas Kashilillah leo amechukua fomu ya kuwania kuteulkiwa kugombea nafasi ya spika katika bunge hilo.


Dar es Salaam. Ikiwa imebaki siku moja ya uchukuaji fomu kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, aliyewahi kuwa Katibu wa Bunge hilo, Dk Thomas Kashilillah amejitosa kwenye kinyang'anyiro hicho.

Dk Kashilillah alikuwa Katibu wa Bunge tangu mwaka 2009 hadi mwaka 2017 baada ya Hayati Rais John Magufuli kumhamisha nafasi hiyo na kumteua kuwa Naibu Katibu wa Wizara ya Kilimo, huku Stephen Kagaigai ambaye sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, akiteuliwa kushika nafasi hiyo.

Leo Januari 14, Dk Kashilillah amefika katika ofisi ndogo ya makao makuu ya CCM jijini Dar es Salaam na kuwa mmoja wa waliochukua fomu ya kuteuliwa na chama hicho kugombea uspika.

Akiwa amevalia shati la Mandela na suruali nyeusi, Dk Kashilillah amefika katika ofisi hizo za CCM saa 3:00 na kuelekea chumba cha Oganizesheni ambako fomu hizo ndipo hutolewa ili kukamilisha taratibu za kuipata ikiwemo malipo ya Sh1 milioni yanayolipwa kupitia benki.

Hata hivyo, alipotoka saa 5:30, alikataa kuzungumza na waandishi waliokuwa katika eneo hilo, akisema sio wakati wake.

Zaidi ya wana CCM 50 wamechukua fomu za kugombea nafasi hiyo.