Dk Mpango kuzindua maabara ya kimataifa Siha
Muktasari:
Makamu wa Rais wa Tanzania, Dk Philip Mpango leo Julai 16,2022 anatarajiwa kuzindua jengo la maabara la kimataifa la afya ya jamii ngazi ya tatu ya usalama ya kibaiolojia Kibong'oto ,Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro.
Siha. Makamu wa Rais wa Tanzania, Dk Philip Mpango leo Julai 16,2022 anatarajiwa kuzindua jengo la maabara la kimataifa la afya ya jamii ngazi ya tatu ya usalama ya kibaiolojia Kibong'oto ,Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro.
Tayari viongozi mbalimbali wakiwamo Serikali wameshawasili katika hospitali hiyo huku shamrashamra zikiendelea nje ya hospitali hiyo.
Pamoja na kuzindua maabara hiyo ambayo ujenzi wake umegharimu Sh12.5bilioni, Julai 18,2022 ataweka jiwe la msingi katika hospitali mpya ya wilaya ya Rombo ambayo ujenzi wake unaendelea na mpaka sasa imegharimu zaidi ya Sh3.49 bilioni.
Maabara hiyo itaweza kutoa huduma za uchunguzi wa magonjwa hasa yanayotishia usalama wa wananchi, taifa na duniani kwa ujumla ikiwemo yanayosababishwa na virusi hatarishi kama ebola, Ukimwi, Uviko -19, dengue, chukungunya, pamoja na magonjwa yanayosababishwa na bakteria.
Kufanya tafiti mbalimbali za ubunifu katika sayansi ya tiba na kinga katika ugunduzi wa dawa vitendanishi, vifaa tiba pamoja na kutengeneza chanjo mbalimbali za kuzuia na kukinga magonjwa ambukizi pamoja na shughuli nyingine.