EAC wakutana kujadili changamoto huduma za posta

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano  na Teknolojia  ya Habari, Mhandisi Kundo Mathew

Muktasari:

Wadau wa Mashirika ya Posta kutoka nchi za EAC wakutana na kujadili namna ya kurahisisha utoaji huduma hizo.

Arusha. Wadau wa mashirika ya posta kutoka nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wamekutana jijini Arusha kujadili changamoto pamoja na kuangalia namna ya kurahisisha utoaji huduma za posta katika Jumuiya hiyo.

Akizungumza leo Novemba  2, 2022 jijini Arusha wakati wa  ufunguzi wa Jukwaa  la Posta Biashara Mtandao na Usafirishaji, Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano  na Teknolojia  ya Habari, Mhandisi Kundo Mathew amesema kuwa, jukwaa hilo lina lengo la kuwakutanisha pamoja wadau hao katika kubadilishana uzoefu na kuweza kuangalia namna bora zaidi ya kuboresha huduma za posta zinazotolewa katika nchi hizo.

Mhandisi Kundo amesema kuwa,jukwaa hilo ni la kwanza kufanyika na wanatarajia kuona huduma zinawafikia  wananchi  kwa haraka zaidi na zenye gharama nafuu na  kuzalisha fursa  ambazo zitawasaidia wateja wa huduma zao.

"Kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira mazuri na rafiki ya kidemokrasia ambapo imetuwezesha sisi kupata fursa ya kuandaa  mkutano huu wa  kwanza wa  watoa  huduma za posta katika nchi za jumuiya. Hiyo ni katika namna ambavyo Rais amekuwa kinara  wa  kuhakikisha mifumo na miundombinu ya  mawasiliano nchini inazidi kurahisishwa,"amesema Mhandisi Kundo.

Ameongeza kuwa, kupitia mkutano huo kuna mabadilishano mengi kwani huduma nyingi sasa hivi zinaenda kidigitali zaidi na tayari posta wameshaanza kutoa  huduma zake kwa njia ya kidigitali zaidi, hivyo wanajivunia  sana kuandaa mkutano huo wa kwanza.

Naye Katibu Mtendaji wa Taasisi ya  mawasiliano ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk Ally Simba amesema kuwa, lengo  ni kuinua na kuipa mwelekeo sekta ya Posta kwani kuna fursa nyingi sana kwenye mambo ya mabadiliko  ya kidigitali, pamoja na biashara  mtandao.

Simba amesema kuwa, kupitia mkutano huo wataweza kuzungumzia jinsi sekta ya posta itasaidia wananchi wake katika uchumi wa kidigitali na matumizi ya fedha pamoja na  masuala ya  biashara mtandao.

Amesema kuwa, hivi sasa katika taasisi ya mawasiliano  ya EAC kuna mchakato unafanywa ili  iwe taasisi ya Tehama ya Afrika Mashariki ili kuhakikisha yale matunda  katika sekta hiyo yaweze kuwafikia wananchi wa jumuiya ya EAC.

Naye Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Macris Mbodo amesema kuwa, ni heshima kwao sekta ya posta Tanzania kushirikiana na taasisi ya posta ya EAC kuweza kuandaa  mkutano wa kwanza wa posta za Afrika Mashariki ambao  haukuwahi kufanyika.

Amesema kuwa,wameona umuhimu wa kukaa pamoja kama wakuu wa  posta za EAC kutafakari namna ambavyo taasisi hizo zitaweza kuendana na mabadiliko ya kiteknolojia na kushiriki mchango katika maendeleo  ya jumuiya ya Afrika  mashariki.

"Namshukuru Rais kupitia mamlaka zake kuturuhusu sisi kufanya mkutano huu,kwani hivi sasa  mageuzi ya posta  yanayoendelea kufanyika yamekuwa vivutio kwa posta zingine za EAC na  kupitia  mkutano huu  tunatumia fursa kuonyesha namna ambavyo tunatoa huduma zetu kidigitali ili na wenyewe waweze kupata uzoefu  katika nchi zao,"amesema

Ameongeza kuwa, huduma zote za posta wameziweka kidigitali hivi sasa na wanasafirisha vifurushi kupitia anuani  za makazi  na wateja wanapelekewa  hadi majumbani kwao.