Eneo laikwaza Moshi kupandishwa hadhi ya jiji
Muktasari:
Hata hivyo, Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tamisemi, Seleman Jafo amesema kigezo muhimu kwa wilaya hiyo ni suala la ukubwa wa eneo ambalo halitoshi
Dodoma. Serikali imesema vikao vyote vya kisheria vya kupendekeza Halmashauri ya Wilaya ya Manispaa ya Moshi kupandishwa hadhi na kuwa Jiji vimeshafanyika.
Hata hivyo, Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tamisemi, Seleman Jafo amesema kigezo muhimu kwa wilaya hiyo ni suala la ukubwa wa eneo ambalo halitoshi.
Jafo ametoa kauli hiyo wakati akijibu swali la Mbunge wa Moshi Mjini, Raphael Michael (Chadema) ambaye alitaka kujua ni lini Serikali itaitangaza Manispaa ya Moshi kuwa Jiji baada ya kukidhi vigezo vyote vinavyotakiwa.
Mbunge huyo amesema halmashauri hiyo ilianza mchakato huo tangu 2012 baada ya kupata baraka za Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete na kuwa vikao vya kamati husika vilishafanyika.
Hata hivyo, Jafo amesema maombi hayo awali yaliwasilishwa na Ofisi ya Rais Tamisemi kwa ajili ya uamuzi, lakini yalirejeshwa ili yafanyiwe marekebisho kutokana na upungufu uliobainika kulingana na vigezo na utaratibu uliopo.
“Hivi sasa timu ya uhakiki kutoka Ofisi ya Rais Tamisemi ina hakiki maombi ya maeneo yote yaliyoomba utawala mpya, ikiwamo Moshi ili kuangalia vigezo vinavyotakiwa,” amesema Jafo.
Kuhusu suala la eneo, amesema manispaa hiyo ina ukubwa wa kilomita za mraba 58 ambalo ni dogo, hivyo wameomba kumegewa eneo la Wilaya ya Hai ili kufikia kilomita za mraba 140.