Kada wa CCM aliyehifadhi viatu vya Mandela afariki dunia
Muktasari:
- Mwenyekiti wa kwanza mwanamke wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Kilimanjaro, Vick Nsilo Swai, amefariki dunia.
Moshi. Mwenyekiti wa kwanza mwanamke wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Vick Swai amefariki dunia.
Vicky aliyekuwa mwenyekiti mwaka 2002 hadi 2012 amefariki dunia jana Jumatatu Mei 31, 2021 baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Mbali na kuwa mwenyekiti wa CCM,Vick atakumbukwa kwa kuhifadhi viatu vya rais wa zamani wa Afrika Kusini, Hayati Nelson Mandela.
Mandela aliviacha viatu hivyo mwaka 1962 alipoingia Tanzania kwa mara ya kwanza akitokea Afrika Kusini ili kuanza harakati za ukombozi, lakini kabla ya kuvichukua alikamatwa na kufungwa gerezani.
Baada ya kutoka gerezani mwaka 1995, Vick alimkabidhi Mandela viatu vyake alivyovihifadhi kwa takribani miaka 30.
Akizungumzia kifo hicho leo Jumanne Juni Mosi, 2021 mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Patrick Boisafi amesema watamkumbuka kwa ushujaa wake kwa kuwa haikuwa rahisi mwanamke kushika nafasi hiyo ya juu kwa vipindi viwili.
Boisafi amesema kwa sasa wanasubiri vikao vya familia yake ndipo zipangwe taratibu za mazishi.