KESI YA MJANE WA BILIONEA MSUYA: Shahidi muuza chips aeleza alivyobadilishana nguo na mshtakiwa
Mke wa marehemu bilionea Erasto Msuya, Miriam Mrita
Dar es Salaam. Katika mwendelezo wa usikilizwaji wa kesi ya mauaji ya Aneth Msuya leo Jumanne, Agosti 22,2023, shahidi ameieleza Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam namna alivyoshiriki katika gwaride la utambuzi wa mshtakiwa wa pili katika kesi ya mauaji hayo.
Shahidi huyo wa 20, Nassib Adrian (47) mkazi wa Njiro Arusha aliieleza mahakama kuwa, pia ameieleza kuwa mshtakiwa huyo Revocatus Everist Muyella alisimama pembeni yake kwamba alibadilishana naye nguo za juu (fulana na shati) kisha shahidi mtambuzi alipopita alimtambua mshtakiwa huyo.
Aneth ambaye aliuawa Mei 25, 2016 nyumbani kwake Kibada, Kigamboni, wilayani Temeke (wakati huo), jijini Dar es Salaam, alikuwa mdogo wa aliyekuwa mfanyabiashara tajiri maarufu wa madini mkoani Arusha, marehemu Erasto Msuya, maarufu kama Bilionea Msuya
Washtakiwa katika kesi hiyo Miriam Steven Mrita, ambaye ni mshtakiwa wa kwanza na mjane Bilionea Msuya aliuawa kwa kupigwa risasi eneo la Mjohoroni, wilayani Hai mkoani Kilimanjaro Agosti 7, 2013; pamoja na Revocatus Everist Muyella (mshtakiwa wa pili).
Kesi hiyo namba 103 ya mwaka 2018 inasikilizwa na Jaji Edwin Kakolaki, na washtakiwa wote wanakabiliwa na shtaka moja tu la mauaji wakituhumiwa kuwa ndio waliohusika katika mauani hayo.
Kwa mujibu wa ushahidi wake, akiongozwa na mwendesha mashtaka, Wakili wa Serikali Marietha Maguta, wakati huo mwaka 2016 alikuwa anaishi Keko Dar es Salaam akijishughulisha na biashara ya kuuza chips anayoifanya mpaka sasa huko Arusha.
Siku ya tukio Agosti 21,2016 alifika katika kituo cha Polisi Kilwa Road, kumfuatilia mtoto wa dada yake aliyekuwa amekamatwa ndipo akaombwa na askari mmoja kushiriki katika gwaride la utambuzi wa mshtakiwa huyo.
Alikubali yule askari alimwelekeza akazunguka nyuma ya kituo hicho ambako aliwakuta watu wengine wanne na baadaye wakaongezeka wengine wakafika wanane, na wote walikuwa wanalingana urefu na kufanana rangi.
Msimamizi wa gwaride aliwalekeza wasimame mstari mmoja, kisha askari mwingine wa kiume alimleta mtuhumiwa akamweleza kuwa anaweza kuchagua sehemu yoyote ya kusimama na kwamba anayo haki hata ya kubadilishana mavazi na watu wengine.
Mtuhumiwa alimuomba naye akamkubalia kubadilishana shati ambapo yeye shahidi alimapatia mtuhumiwa fulana yake ana yeye akavaa ya mtuhumiwa.
Mtuhumiwa alisimama pembeni yake akiwa wa nane kutoka mkono wa kulia na yeye shahidi akiwa wa tisa.
Halafu askari mmoja wa kike alimleta dada mmoja mfupi mwenye rangi ya maji ya kunde, akafahamisha kwamba kuna gwaride la utambulisho kumtambua mtuhumiwa wake.
Yule dada alielezwa kuwa apite mbele yao na kama atamtambua mtuhumiwa wake amshike bega kwa nyuma. Alianza kupitia mbele yao kisha akaenda nyuma yao ndipo akamshika bega mtuhumiwa, ambaye alikuwa wa pili kutoka kushoto.
Mkaguzi wa gwaride alkmuuliza huyo dada kama ana hakika kuwa aliyemgusa ndiye huyo naye akasema kuwa ndiye huyo. Hivyo askari alichukua karatasi akaandika majina na kuwasainisha, wote walioshiriki gwaride pamoja na askari huyo.
Baada ya hapo askari wa kike alikwenda kuchukua yule dada halafu askari mwingine wa kiume akamchukua mtuhumiwa wakaondoka.
Wakili Maguta: Huyo mtuhumiwa aliyeletwa hapa yuko wapi?
Shahidi: Naomba yule mtuhumiwa pale avue barakoa ili niweze kumtambua kama ndiye yeye au siye
Jaji: Haya uliyevaa barakoa kama kuna mtu amevaa barakoa humu aivue ili shahidi amtambue
Mshtakiwa wa pili, Muyea anavua barakoa
Shahidi: Ni yeye huyo ila sasa hivi amepungua sana.
Jaji: Ni yupi Sasa?
Shahidi: Ni huyo aliyevaa miwani
Wakili: Hebu nenda umuoneshe
Shahidi anakwenda kumshika mshtakiwa wa pili.
Baada ya ushahidi wake huo wa msingi alihojiwa na mawakili wa utetezi, Peter Kibatala na Nehemiah Nkoko.
Kibatala: Shahidi una elimu gani?
Shahidi: Elimu yangu darasa la Saba
Kibatala: Unafahamu maana ya certification?
Shahidi: Sifahamu
Kibatala: Maana ya participant?
Shahidi: Sifahamu nimekwambia elimu yangu darasa la Saba
Kibatala: Sikiliza swali shahidi. (Anampa fomu aliyosaini wakati wa gwaride la utambuzi kisha anaendelea kumuuliza maswali). Hapa kuna mshtakiwa anaitwa Revocatus Everist Muyella, Kwenye hii fomu tafuta jina Muyella.
Shahidi: Sioni Muyella
Kibatala: Umeiambia Mahakama lini ulihamia Arusha?
Shahidi: Sikuiambia
Kibatala: Huyu mshtakiwa alikuwa anaishi Arusha, ulitambua hilo?
Shahidi: Hapana
Kibatala: Ulimwambia Mheshimiwa Jaji kwamba kwenye lile gwaride hapakuwa na askari mwingine isipokuwa Mkaguzi?
Shahidi: Sikumwambia
Kibatala: Ulimwambia Jaji kuwa yule mtuhumiwa aliyekuja hakuwa na pingu kiasi hivyo ilikuwa rahisi kumtambua?
Shahidi: Sijamwambia
Kibatala: Umesema.kuwa ulibadilishana shati na mtuhumiwa, uliieleza Mahakama ilikuwa ni ya rengi gani?
Shahidi: Sijamwambia
Kibatala: Wewe una urefu gani?
Shahidi: Futi Tano
Kibatala: Unafahamu mtuhumiwa ana futi Sita?
Shahidi: Ndio nafahamu?
Kibatala: Wewe futi 5 na yeye futi 6 bado unasema urefu mlikuwa mnalingana?
Shahidi: Ndio
Kibatala: Ulimwambia Jaji kuwa mtuhumiwa naye alisaini ile karatasi?
Shahidi: Sikumwambia
Kibatala: Umesema hujui Kiingereza, wapi ulimwambia Jaji kuwa afisa yule aliyekuwepo kwenye gwaride au yeyote alikutafsiria yaliyomo kwenye hii fomu?
Shahidi: Sikumwambia
Nkoko: Shahidi nashukru umemjibu vizuri Wakili Kibatala, ulisema mtuhumiwa anakuzidi urefu?
Shahidi: Ndio
Nkoko: Kwa hiyo wote Tisa (walioshiriki gwaride la utambuzi) mlikuwa mnalingana urefu na rangi?
Shahidi: Ndio lakini sasa hivi mimi nimenenepa nimeshuka kidogo (jibu hilo linaqafanya watu waliokuwemo ndani kuangua vicheko)
Nkoko: Shahidi hunaiambia Mahakama kwamba wote Tisa kwenye parade mlikuwa mmevaa mavazi yanayofanana?
Shahidi: Ndio
Nkoko: Umeiambia Mahakama kuwa zoezi la utambuzi lilianza muda wa saa 5, ni sawa?
Shahidi: Ndio
Nkoko: Wala hujasema liliisha saa ngapi?
Shahidi: Ndio
Nkoko: Hebu angalia hii karatasi, soma nyuma (anamuonesha) zoezi lilianza saa 6:45.
Shahidi: Labda nifafanue...
Nkoko: Mimi sitaki ufafanuzi iutampa mwendesha mashtaka, mimi nataka ndio au Hapana. Kwa hiyo wewe unasema saa 5, kielelezo kinasema saa 6 sasa huoni kama ulikuwa unaidanganya Mahakama?
Shahidi: Hapana, mimi nilisema.nilifika saa 5..
Nkoko: Mimi sihitaji ufafanuzi Kwa hiyo Mahakama ichukue yapi kati ya maneno yako na ya kielelezo?
Shahidi: Mahakama ina mkondo wake wa kufanya kazi imi siwezi kuingilia
Nkoko: unakumbuka uliandika maelezo yake tarehe 21 mwezi wa 8, 2016?
Shahidi: Ndio
Nkoko: Wakati ule unaandika maelezo bila shaka ulikuwa bado na kumbukumbu nzuri kuliko sasa?
Shahidi: Ndio kama nitasahau ni kidogo sana.
Nkoko: Anasoma nakala ya maelezo kisha anampa na anamuuliza kama anayatambua kutokana jina na saini kuwa ni yake?
Shahidi: Ndio nayatambua.
Nkoko: Nilikuuliza swali hapa kwamba wewe ulisimama eneo gani ukasema wa kwanza kutoka kushoto, sasa hebu soma hapa (anamuonesha shajidi sehemu ya kusoma katika maelezo yake hayo ya maandishi)
Shahidi: Mimi ni mbovu wa macho.
Nkoko: Anasoma sehemu hiyo....mimi nilikuwa wa kwanza kutoka kulia...kisha anamuuliza; unakubaliana na mimi kuwa maelezo yako ya sasa ni ya uwongo?
Shahidi: Hapo kaandika mwanadamu kukosea ni kawaida.Nkoko: Ulisema wote mliosimama katika mstari mlikuwa mnalingana kimo na rangi, kwenye haya maelezo ni wapi imeandikwa hiyo?
Shahidi: Hiyo sikumwambia ila (askari aliyeandika maelezo yake) ni katika utashi wangu kama nilivyoona.
Nkoko: Kwa kuwa maelezo yako haya ni tofauti na uliyoyaandika ungependa Mahakama iyapilokee ili ione tofauti hizi wakati inaandika uamuzi?
Shahidi: Mahakama ndio itaona lakini mimi huu ndio ushahidi wangu.
Baada ya mahojiano hayo mwendesha.mashtaka, Wakili Maguta alimhoji maswali ya.kumuongoza kusawazisha hoja zilizoibuliwa kwenye maswali ya dodoso, kwa kufafanua baadhi ya majibu yake.
Wakili Maguta: Shshidi, Wakili alikupa kielelezo hiki ( hati ya gwaride la utambuzi) na akakuuliza kam kuna jina Revocatus Everist Muyella, ukajibu kuwa halipo, hebu fafanua hapa lipo au halipo?
Shahidi: Lipo lakini ubini haupo.
Wakili: Limeandikwaje?
Shahidi: Revocatus Evaruti
Wakili: Limeandikwaje?
Shahidi: Evaruti
Jaji: Hebu nione ( anaangalia.kisha anamrudishia PP)
Wakili: Pia Umeulizwa kuwa mshtakiwa ana futi 6 na wewe futi 5 ukaulizwa kama mnalingana, hebu fafanua.
Shahidi: Nimesema wakati ule tulikuwa tunalingana lakini sasa hivi baada ya kunenepa nikadidimia kidogo
Wakili: Shahidi umeulizwa kama mtuhumiwa alikuwa na pingu hebu fafanua Hilo.
Shahidi: Hakuwa na.pingu.
Awali amepanda kizimbani shahidi wa 19, Aziza Shaban Hassan. Huyu ni mtoto mwenye umri wa miaka 16 Mkazi wa Kibada Kigamboni Block namba 16 na mwanafunzi wa kidato cha Tatu.
Hata hivyo kabla ya kutoa ushahidi wake akiongozwa na karani kuahidi kusema ukweli kama Sheria ya Ushahidi inavyoelekeza kwa Sasa Kwa ushahidi wa mtoto badala ya kula kiapo.
Kwa mujibu wa usjahidi wake akiongozwa na mwendesha mahtaka, Wakili wa Serikalj Generose Montano, Mei 25, 2016 wakati anarudi kutoka shuleni muda wa saa10 jioni, alikutana na dada mmoja mfupi na mwenye rangi ya maji ya kunde.
Dada huyo ambaye hakumtaja kina alimkabidhi ufunguo akamwelekeza aupeleke katika nyumba ya jiraninyao Kibada Block namba 17 na baada ya kuikabidhi ifuo hil aliondoka akaenda nyumbani kwao.
Ifuatayo ni sehemu mahojiano yake na Wakili Kibatala:
Kibatala: Shahidi Nimekusikia ukisema kuwa umri wako ni miaka 16, ni sahihi?
Shàhidi: Ndio
Kibatala: Kwa hiyo wewe ni mtoto?
Shahidi: Ndio
Kibatala: Sàsa Aziza kabla ya kuapa au kabla dada hajakuuliza maswali ulimsikia alikuuliza.kama.unaelewa maana ya kiapo?
Shahidi: Hapana
Kibatala: Ulishawahi kuapa mahali.pengine popte?
Shahidi: Ndio
Kibatala: Ulimwambia Jaji kuwa ulishawahi kuapa.mahali.pengine?
Shahidi: Hapana
Kibatala: Ulisema kuna dada alikupa ufunguo?
Shahidi: Ndio
Kibatala: Lakini humfahamu
Shahidi: Ndio
Kibatala: Na hujaulizwa (na wendesha mashtaka) kama.ulimuulza ni nani?
Shahidi: Ndio
Kabla ya kuanza kusikiliza ushahidi wa mashahidi hao Kiongozi wa jopo la waendesha mashtaka, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Paul Kimweri ameieleza.mahakama kuwa wamewasilisha taarifa ya nia ya kumuongeza shahidi mmoja.
Hoja hiyo ilipangwa vikali na Mawakili wa utetezi, Peter Kibatala na Nehemia Nkoko na hivyo kuibua mvutano mkali wa hoja za kisheria, kabla ya Mahakama kuandika na kutoa uamuzi wake. Mvutano huo wa hoja ulikuwa kama ifuatavyo:
Wakili Kimweri: Mheshimiwa Jaji kabla ya kumuita shahidi tunaomba ikae kwenye rekodi kwamba Agosti 21, 2023 upande wa mashtaka tulileta mahakamani ilani chini ya kifungu cha 289(1), (2), (3),(4) CPA, tukiitaarifu mahakama kwamba tuna nia ya kuleta shahidi wa nyongeza mmoja anayeitwa Dk Hassan Chande wa kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Substance (msingi) ya ushahidi wake ni kwamba ndiye aliyeandaa taarifa ya uchunguzi wa kifo cha marehemu Aneth Msuya, ambayo ilishawahi kupokewa kama kielelezo wakati wa PH (usikilizwaji wa awali).
Kibatala: Mheshimiwa Jaji sisi tuna mambo mawili , kwanza kwa sababu hiyo notice ni discretion (hiyari) ya Mahakama chini ya kifungu husika, lakini tunaomba mahakama iangalie reasonability(umaana ) ya hii notice.
Pili, wenzetu wametupatia notice lakini hawajatupa statement ( maelezo ya maandishi ) ya huyu shahidi. Tunaomba watupatie nakala yake.
Nkoko: Mheshimiwa Jaji kifungu cha 289 kinasema wazi kuwa shahidi ambaye hakuwa listed (hakuorodheshwa) na statement yake haikusomwa wakati wa committal anaweza kuruhusiwa tu baada ya notice.
Sasa hawa wametu-surprise (wametushtukiza kutuletea leo notice bila statement ya huyo shahidi.
Kwa sababu kifungu cha 246 hakikuzingatiwa tunaomba kama wana shahidi mwingine wamlete tuendelee naye huyu waende kwanza wakatufute statement kwani matakwa ya sheria yanazuia shahidi ambaye statement yake haikusomwa kwenye committal.
Wanapaswa waje waieleze ni lini walipata ufahamu kwamba shahidi huyu anapaswa kuja kutoa ushahidi.Sisi tunafahamu kwamba ufahamu waliupata siku waliyopata kielelezo hiki.
Na kesi zinazofanyika HQ (Mahakama Kuu) si siri maana washtakiwa wanapaswa kupewa kila kitu kujua status ya kesi inavyoendelea. Kwa hiyo ni rai yetu hatukai tumepokea notice lakini watuletee hiyo statement.
Kimweri: Kifungu hiki kinahusiana na shahidi wa nyongeza ambaye maelezo yake hayapo au hayajawahi kusomwa au hayakurekodiwa.
Kwa hiyo statement ya shshidi huyo wasiilazimishe kwamba lazima iwepo maana kifungu chenyewe kinajieleza kwamba ni kwa shahidi ambaye statement yake haipo kwa sababu yoyote ile. Kwa hiyo wakielewe kwanza hicho kifungu.
Ni kwa msingi huo ndio maana hoja wanayoileta wenzetu kifungu hiki hakina matakwa ya huyo shahidi anayeongezwa iambatanishwe na statement ma hii si kwa bahati mbaya ni kwa sababu ni statement ambayo haipo kwenye kumbukumbu za mahakama.
Kwa hiyo wasitegemee kwamba tuna statement ya kuambatanisha,hatuna na sheria hailazimishi hilo.
Matakwa ya kifungu hiki ni kuleta notice ikitaja jina na substance ya ushahidi wa shahidi anayekusudiwa kuongezewa.
Hayo ndio masharti ambayo yamewekwa na kifungu kidogo cha (2).Suala la reasonability na time ni la Mahakama kwa mujibu wa kifungu kidogo cha (3). Kwa hiyo hatuoni chochote ambacho tumekikikiuka.
Kibatala:Kwa kuwa substance ya ushahidi wake haikusomwa kwenye committal unapoleta notice lazima na substance ya ushahidi wake iletwe. Na sijui kwanini zinatoka arrogance statement kwamba wenzetu wsitegeme kuwa tuta-supply (tutaitoa) hiyo statement na haipo badala ya kutoa hoja za kisheria.
Kwa hiyo Mheshimiwa Jaji wakati unaandika ruling (uamuzi) tunaomba na hiyo izingatiwe hata kama hakuna shahidi huyo leo.
Hata hivyo Jaji Kakolaki baada ya kusikiliza hoja za pande zote katika uamuzi wake alikubaliana na taarifa ya upande wa mashtaka akaridhia shahidi huyo kuitwa wakati wake utakapofika.
Kesi hiyo inaendelea tena Leo kwa mashahidi wengine wa upande wa mashtaka.