Kitakachotokea Musiba akishindwa kumlipa Membe

Muktasari:

  • Hukumu ya kesi ya madai ya kashfa iliyofunguliwa na Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe dhidi ya Cyprian Musiba anayejitambulisha kama mwanaharakati huru, inafikisha jumla ya fidia anazotakiwa kulipa kuwa takriban Sh18.58 bilioni.


Dar es Salaam. Hukumu ya kesi ya madai ya kashfa iliyofunguliwa na aliyekuwa Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe dhidi ya Cyprian Musiba anayejitambulisha kama mwanaharakati huru, inafikisha jumla ya fidia anazotakiwa kulipa kuwa takriban Sh18.58 bilioni.

Kiasi hicho anachotakiwa kuwalipa watu aliowakashfu kupitia vyombo vyake vya habari ndani ya miaka sita iliyopita kinamweka katika hatari ya kufungwa jela iwapo atashindwa kukilipa, mawakili wamesema.

 Mahakama Kuu ilimwamuru Musiba kumlipa Membe jumla ya Sh6 bilioni baada ya kumshinda katika kesi ya madai ya kashfa aliyomfungulia.

Mbali na Membe, wakili maarufu nchini, Fatma Karume alisema Mahakama Kuu Zanzibar ilimwamuru Musiba amlipe Sh12.5 bilioni kwenye kesi yake ya madai ya kashfa aliyomfungulia.

Vilevile, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilishamwamuru Musiba kumlipa waziri wa zamani wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka fidia ya Sh80 milioni kutokana na kashfa alizozitoa dhidi yake.

Hata hivyo, katika hukumu ya kesi ya Membe, kupitia wakili wake Mushumba Cosatta, Musiba alisema wanakusudia kukata rufaa kupinga hukumu hiyo, wanasubiri kupata nakala ya hukumu ili waandae sababu za rufaa.

Baadhi ya mawakili walisema endapo Musiba atashindwa kulipa fidia hiyo na hatakuwa na mali za kupigwa mnada kufidia kiasi hicho basi wanaomdai wanaweza kuomba mahakama imfunge kama mfungwa wa madai.

Akitoa maoni kuhusu hukumu hiyo, Wakili Fulgence Massawe alisema kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Madai (CPC), wanaomdai wanaweza kuiomba mahakama impeleke jela na watakuwa wanamlipia gharama kwa muda wote atakaokuwa gerezani.

“Gharama hizo zitakuwa zinajumlishwa kwenye deni analodaiwa,” alisema.

Naye John Seka alisema mfungwa wa madai hutumikia kifungo kwa kipindi cha miezi sitasita. “Aliyemfunga anaweza kuongeza muda kila unapoisha hadi mdaiwa atakapokubali kulipa deni lote.”