Latra yajipanga kupiga mnada bajaji korofi

Wakazi wa Jiji la Arusha wakitumia usafiri wa gari ndogo la mizigo kutokana na mgomo wa madereva wa daladala wakishinikiza kuondolewa kwa bajaji katika njia wazazozitumia. Picha na Bertha Ismail

Arusha. Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (Latra), imeanza mchakato kuomba ruhusa ya Mahakama ya kuzipiga mnada bajaji zitakazomatwa zaidi ya mara moja zikiendesha shughuli zake bila leseni.

Hayo yameezwa na ofisa mfawidhi wa Latra, Mkoa wa Arusha, Amani Mwakalebela alipokuwa anazungumzia suluhu ya mgomo wa wenye daladala ulioanza alfajiri ya jana kushinikiza bajaji ziondolewe kwenye barabara walizopangiwa.

Alisema ndani ya Jiji la Arusha kuna zaidi ya bajaji 2,000 zinazofanya kazi, wakati zilizosajiliwa hazizidi 350.

“Kama mnavyojua awali waliokuwa wanatoa leseni za usafirishaji ni halmashauri ya Jiji la Arusha, lakini tangu mwaka jana tulikaa na tukaamua tufunge usajili baada ya kuonekana zimekuwa nyingi, lakini nashagaa pamoja na kufunga, bado kuna baadhi ya wafanyabiashara wameendelea kuzinunua na kuziingiza katika mzunguko," alisema.

Alisema baada ya kuona hivyo, waliamua kufanya operesheni maalumu ya kuzikamata na kuzipiga faini huku wakiwataka wamiliki wake wahamie maeneo mengine, ikiwemo miji isiyo na bajaji kabisa, lakini wamekaidi.

"Si kwamba hatuwakamati au kuwapa adhabu, tunafanya hivyo lakini hawasikii. Mtu leo analipa faini kesho yuko barabarani, hivyo tumeanza mchakato wa mahakama kuomba oda ya kuzichukua kabisa zisiwepo kwenye mzunguko na kuzipiga mnada mbali kabisa,” alisema.

Mwakalebela alitumia nafasi hiyo kuwaomba madereva wa daladala kupitia uongozi wao kurudi barabarani na kuendelea kutoa huduma wakati suala la bajaji likiendelea kufanyiwa kazi.

Akizungumzia mgomo huo, mmoja wa madereva wa daladala, Emmanuel Swai alisema wameamua kugoma kutokana na uonevu unaofanywa na mamlaka za usafirishaji, kwa kuziruhusu bajaji kufanya kazi kwenye njia wanazotoa huduma, hasa barabara za Uswahilini-Dampo, Sombetini-Ngusero-Majengo pamoja na na Patel-Kwa Mrombo.

"Awali makubaliano ilikuwa ni bajaji zinakaa eneo moja kama teksi wakodishwe wapeleke watu mahali, lakini sasa hivi wanafanya kazi ya kuokota abiria kama sisi wa daladala, tena wanakaa kwenye maegesho yetu na zaidi wanapita ruti zilezile tunazopita, kitendo ambacho kinatuharibia biashara,” alisema.

Akizungumzia mgomo huo, mwenyekiti wa Chama cha Wasafirishaji Mkoa wa Arusha na Kilimanjaro (Akiboa), Locken Adolf alisema utitiri wa bajaji umeathiri biashara ya daladala, hivyo wanaiomba Serikali kuzipunguza barabarani.

“Kwa ukubwa wa eneo la Arusha, (bajaji) hazitakiwi kuzidi 100, lakini sasa zimekuwa nyingi na zimekuwa kero hasa baada ya kuteka njia zote za daladala na zinafanya biashara ya kuokota abiria kama wanavyofanya wenzao, tofauti na makubaliano wakati zinaingia mjini," alisema.

Akizungumzia hali hiyo, Amina Hassan alisema kuwa mgomo huo ulianza leo alfajiri umesababisha mateso makubwa kwa wakazi wa Jiji la Arusha pamoja na wanafunzi wanaotumia usafiri huo kuwahi makazini na shuleni.

Ramadhani Ally aliiomba Serikali kusikiliza madai ya daladala endapo yana mantiki yapatiwe suluhisho na kama hayana basi waondolewe na magari makubwa aina ya Toyota Coaster yaletwe yachukue nafasi yao.

"Shida hawa (wenye) daladala wanataka wenyewe ndiyo wafanye kazi ya usafirishaji wakati hii ni biashara huria, inafaa kila mtu acheze kwenye nafasi yake kupata kipato, tunaiomba Serikali isikize madai yao, kama yana maana wyatatuliwe lakini kama ni haya ya ubinafsi ili wenzao wasifanye kazi, basi wanaohamasisha mgomo wafutiwe leseni," alisema.