Lifti yaporomoka Dar, yajeruhi watano

Mlango wa chini kuingia kwenye lifti iliyoporomoka katika jengo la ghorofa la Millenium ‘Millenium Tower’ lililopo Makumbusho, jijini Dar es Salaam.

Muktasari:

  • Lifti iliyopo katika jengo la Millenium Tower, Makumbusho, imeporomika na kujeruhi watu kadhaa waliokuwa wakiitumia.

Dar es Salaam. Lifti iliyopo katika jengo la ghorofa la PSPF ‘Millenium Tower’ Makumbusho, jijini hapa, imeporomoka na kujeruhi watu watano huku timu inayochunguza chanzo cha ajali hiyo ikiwa inaendelea na kazi eneo la tukio.

Akizungumza kwa simu na Mwananchi Digital, Kamishna Msaidizi Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Kinondoni (ACF) Christina Sunga amethibitisha kes kusema kuwa: “Ni kweli tukio hilo limetokea jengo la PSPF Millenium Tower hapo Kijitonyama, lift imeporomoka kama mlivyopata taarifa, na tunaendelea kuchunguza chanzo cha ajali hiyo."

Kwa mujibu wa Kamishna Msaidizi  Sunga, timu ya Zimamoto na Ukoaji ilifika muda mfupi baada ya tukio kutokea na kukuta baadhi ya watu waliokuwemo kwenye lift hiyo, wakiwa wameishapewa msaada na kuondoka eneo hilo, hata hivyo, watu watano walionekana kuihitaji msaada wa huduma za afya na hivyo kumbikizwa Hospitali ya Kairuki iliyo karibu na eneo hilo.

"Kikosi chetu cha Zimamoto na Uokoaji kilifika eneo la tukio muda mfupi sana baada ya ajali kuokea na kupewa taarifa. Tulikuta watu wengine wameishaokolewa, hata hivyo; watu watano tuliwakimbiza hospitali hapo Kairuki kwa msaada zaidi wa kitabibu, na kimsingi wanendelea vizuri. Timu yetu bado inaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha ajali hiyo," amesema Sunga, na kuongeza kuwa:

"Taarifa kamili juu ya chanzo cha ajali na idadi ya watu waoikuwa ndani ya lifti hiyo tutawapa mara baada ya uchunguzi kukamilika. Timu inafuatilia picha za CCTV cameera za jengo husika, lakini pia mfumo wa lifti hiyo na hivyo kubaini chanzo cha ajali."

Hata hivyo, awali Mkaguzi Msaidizi wa Jeshi hilo Patrick Afande alinukuliwa akiambia runinga ya TBC kuwa chanzo cha lifti hiyo kuporomoka ni kuzidisha idadi ya watu kinyume na uwezo wake ambapo wakati tukio hilo linatokea inasemekana ilibeba zaidi ya watu 10.

Na kwamba lifti hiyo iiliporomoka kutoka ghorofa ya 10 na kujeruhi watu kadhaa ambao kwa mujibu wa Kamanda huyo, wamepelekwa katika hospitali ya Kairuki, kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

Taarifa za awali zilionyesha kuwa ajali hiyo ilisababishwa na na lifti husika kushindwa kuhimili uzito mkubwa wa watu kinyume na kiwango chake, kitu ambacho ACF Sanga anataka wadau wasubiri matokeo ya uhakika toka timu ya uchunguzi.

Kwa habari zaidi endelea kutufuatilia Mwananchi.