Lukuvi apiga marufuku kodi ya miezi sita NHC

Muktasari:

Alitaka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuwapangisha wananchi kwenye nyumba zake na kuwadai kodi ya mwezi mmoja na si zaidi ya miezi sita.


Moshi. Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amepiga marufuku Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kutumia madalali kupangisha nyumba zake na kuwadai kodi ya zaidi ya miezi sita.

Waziri Lukuvi alitoa agizo hilo jana wakati akizungumza na watumishi wa NHC mkoa wa Kilimanjaro.

Alisema ni marufuku kwa baadhi ya watumishi wa shirika hilo kutumia vishoka na kulazimisha wananchi kulipa kodi ya nyumba kwa zaidi ya miezi sita.

Lukuvi alisema Serikali inakemea vikali na haitavumilia kuona tabia ya watumishi wa shirika hilo wakidai wananchi kodi ya zaidi ya miezi sita.

"Hii tabia Serikali tunaikemea na hatupendi kuona wananchi maskini wakinyanyasika katika nchi yao," alisema Lukuvi.

Waziri huyo alisema shirika hilo linatakiwa kuonyesha mfano bora wa kupangisha na kudai kodi ya mwezi mmoja tofauti na wapangishaji binafsi wanaodai kodi kwa maskini ya zaidi ya miezi 12.

"Ningependa shirika la nyumba muonyeshe huduma ya mfano bora wa kupangisha na kudai kodi ya mwenzi mmoja tofauti na wapangishaji binafsi wanadai maskini kodi ya zaidi ya miezi sita," alisema Lukuvi.

Awali, Meneja wa NHC mkoani humo, Juma Kiaramba alisema kwa mwaka 2017/18 walifanikiwa kukusanya Sh2.8 bilioni sawa na asilimia 100.58.

"Kutokana na utaratibu mzuri wa ukusanyaji wa kodi zetu tumefanikiwa kukusanya Sh.2.82 bilioni mwaka wa fedha ulioisha Juni wa 2017/18.”

“Tulifanya ukarabati wa majengo yetu kwa kutumia Sh255 milioni hadi sasa tunadai wapangaji wetu Sh54 milioni," alisema Kiaramba.

Alisema shirika hilo litaanza kujenga nyumba 25 za gharama nafuu na tayari wametenga kiasi cha Sh1.4 bilioni ambapo itachukua miezi 18 kuanzia sasa.