Mahakama ya Afrika yatoa hukumu 17, sita za Tanzania

Baadhi ya majaji wa mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu wakitoa maamuzi ya hukumu 17 zilizowasilishwa mahakamani hapo. Picha na Janeth Joseph

Muktasari:

Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu imeweka rekodi kwa mara ya kwanza baada ya kutoa uamuzi wa hukumu 17 kwa mpigo tangu kuanzishwa kwake miaka 15 iliyopita.

Arusha. Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, leo Alhamisi Septemba 22, 2022 imetoa hukumu ya mashauri 17 yaliyowasilishwa katika Mahakama hiyo, miongoni mwa mashauri hayo sita ni kutoka Tanzania.

Katika mashauri hayo sita, manne yalitupiliwa mbali kutokana na kuwasilishwa nje ya muda.

Moja ilikuwa haina mashiko, ya sita pamoja na kuwa hoja zake nyingi zilitupiliwa mbali Mahakama ilikuta haki zake za kupewa wakili zilikiukwa hivyo Serikali ya Tanzania kutozwa fidia ya 600,000 ambazo inatakiwa ilipe ndani ya miezi sita.

Uamuzi huo umetolewa leo Alhamisi Septemba 22, 2022 na jopo la majaji 10 wa Mahakama hiyo yenye makao yake makuu jijini Arusha.

Miongoni mwa mashauri yaliyowasilishwa katika mahakama hiyo ni kesi za makosa ya jinai, ukiukwaji wa haki za binadamu ikiwemo kufukuzwa kazi pamoja na mambo  mengine.

Akizungumza mara baada ya kutolewa kwa maamuzi hayo, Rais wa mahakama hiyo, Jaji Iman Aboud amesema mahakama hiyo kwa mara ya kwanza imeweka rekodi ya kutoa huku nyingi kuliko kipindi kilichopita huku akisema ni kutokana na majaji kufanya kazi kama timu moja.

"Leo mahakama hii imehitimisha kikao chake cha 66 ambacho kimekaa kwa muda wa wiki nne na kufanikisha kutoa uamuzi wa hukumu 17.

“Kikao ambacho tumeweza kutoa hukumu nyingi zaidi na hii imeweka rekodi, tunasema ni kwa sababu tunafanya kazi kama timu moja na kuzingatia misingi yetu ya kazi kama majaji," amesema Jaji Aboud