Mali za Impala Hotel kuuzwa kulipa wafanyakazi

Mali za Impala Hotel kuuzwa kulipa wafanyakazi

Muktasari:

  • Mali za Kampuni za hoteli maarufu za kitalii za Impala na Naura Spring Hotel zinatarajiwa kuanza kuuzwa wiki ijayo ili kulipa Sh1.2 bilioni wanazodai wafanyakazi.

Arusha. Mali za Kampuni za hoteli maarufu za kitalii za Impala na Naura Spring Hotel zinatarajiwa kuanza kuuzwa wiki ijayo ili kulipa Sh1.2 bilioni wanazodai wafanyakazi.

Mali hizo zinauzwa baada ya kampuni ya Impalla kufikia makubaliano na  Kamishna wa Kazi leo Ijumaa Septemba 10, 2021 katika Mahakamani kuu kitengo cha Kazi .

Mkataba wa Maridhiano ya uuzwaji wa mali za kampuni hiyo umefikiwa ili waweze kupata fedha za kulipa madeni ambayo waliyalimbikiza kwa kutowalipa  wafanyakazi hoteli za kitalii  za Naura Spring na Impala ambao hawajalipwa kwa muda mrefu.

Kufuatia hatua hiyo Mahakama Kuu kitengo cha Kazi imemwamuru Dalali wa Mahakama kuanza utekelezaji wa uuzwaji wa mali hizo na hadi kufikia Octoba 15, 2021 wafike Mahakamani wakiwa na majibu ya wafanyakazi wote kulipwa.

Mali ambazo kampuni ya Impala na Kamishna wa kazi wameziwasilisha mahakani hapo na kupewa ridhaa na Naibu msajili mahakama kuu Kanda ya Arusha, Ruth Masam ni viwanja ambavyo vipo katika kiwanja namba 16 mpaka 23 katika eneo la uzunguni corido Area A Jijini Arusha .

Katika malipo hayo wafanyakazi kutoka katika kampuni zote mbili wanatarajia kupata zaidi ya Sh1.2 bilioni mbapo wafanyakazi wa Impalla  watalipwa Sh787.5 milioni  na  Naura Spring hotel watalipwa milioni Sh180.9 milioni

Fedha nyingine zinatarajiwa kulipwa mifuko ya ya hifadhi ya jamii kama mafao ya wafanyakazi na gharama za shauri hilo.

Jumla ya wafanyakazi  wanaodai madeni hayo Naura ni wafanyakazi 68 na Impala  hoteli 165 mgororo huo ulianza tangu mwaka 2019.