Mrema, Dk Magufuli wapigiana kampeni Vunjo

Mgombea urais wa CCM, Dk John Magufuli (Kushoto) akisalimiana na Mwenyekiti wa TLP taifa, Augustino Mrema.  Picha na Adam Mzee

Muktasari:

Dk Magufuli aliongeza kuwa kama wananchi wa Vunjo hawatamchagua Shirima au Mrema watapata shida kwani aliwaita wagombea wengine kuwa ni wababaishaji.

Rombo na Vunjo. Katika hali ambayo haikutarajiwa, Mwenyekiti wa TLP taifa, Augustino Mrema jana amemnadi mgombea urais wa CCM, Dk John Magufuli kuwa  ndiye anafaa kuwa rais wakati chama chake kikiwa kimemsimamisha, Macmillian Lyimo kuwania nafasi hiyo  ya urais kwa tiketi ya TLP.

Hali hiyo ilianza kwa Dk Magufuli kumpigia debe Mrema anayewania ubunge Jimbo la Vunjo kwa tiketi ya TLP kwa kusema kuwa ana historia nzuri na uzoefu katika uongozi kuliko wengine.

Dk. Magufuli alisema hayo  hiyo jana wakati akihutubia wananchi katika Uwanja wa Polisi Himo ambapo alisema wananchi wasikosee kwenye kupiga kura na kuwa hata kama hawaitaki CCM, basi wampigie kura Mrema.

“Kama humtaki mgombea wa CCM wa jimbo hilo, Innocent Shirima angalau mniletee Mrema,” alisema Dk Magufuli na kuongeza hata msahau Mrema bali atamtafutia kazi nyingine.

Dk Magufuli aliongeza kuwa kama wananchi wa Vunjo hawatamchagua Shirima au Mrema watapata shida kwani aliwaita wagombea wengine kuwa ni wababaishaji.

Akiomba kura kwa wananchi katika mkutano huo, Shirima mwenyewe alisema endapo atachaguliwa atahakikisha kero ya barabara za Kilema, Mua, Himo, Saidingi, Kahe na Chekereni zinatengenezwa.