Msechu apunguza kilo saba, aweka rekodi

Muktasari:

  • Msechu amefanikiwa kupunguza uzito wa kilo saba ndani ya siku saba tangu awekewa puto tumboni na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Mloganzila.

Dar es Salaam. Msanii Peter Msechu amefanikiwa kupunguza uzito wa kilo saba ndani ya siku saba tangu alipowekewa puto na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Mloganzila ili kumsaidia kupunguza uzito.

 Msechu aliwekewa puto hilo Januari 25, 2023 akiwa na uzito wa kilo 143.4 lakini kufikia leo Februari Mosi 2023, ana uzito wa kilo 136.5, wastani wa punguzo la uzito la kilo moja kila siku.

Kwa mujibu wa taarifa iliyowekwa leo kwenye ukurasa wa Instagram wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Mloganzila, imethibitisha kwamba msanii huyo wa Bongo Flava amepunguza uzito huo ndani ya muda mfupi.

“Msanii Peter Msechu amepungua kilo saba, toka afanyiwe huduma tiba ya kuwekewa puto (intragastric balloon) kwenye tumbo la chakula ili kumsaidia kupungua. Huduma hiyo alifanyiwa Januari 25, 2023, katika Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila,” inaeleza taarifa hiyo.

Msechu pia ameandika katika ukurasa wake wa Instagram kuonyesha kwamba amepunguza uzito huo huku wakiwashukuru madaktari wa Hospitali ya Muhimbili Mloganzila kwa kufanikisha azma yake ndani ya muda mfupi.

“Eeeh Mwenyezi Mungu sijui nikushukuru vipi, niliwekewa puto Januari 25, 2023, picha hiyo nilipiga asubuhi wakati naenda hospitali asubuhi. Leo ni siku ya saba baada ya kumeza puto Februari Mosi, 2023 nimepiga picha hiyo muda ule ule wa asubuhi kama wakati naenda hospitali. Nimepunguza kilo saba kwa siku saba, ina maana kila siku kilo moja inazikwa. Muhimbili hii mmetishaa.

“Kipekee kabisa asanteni sana wataalamu wote na madakatari kutoka Hospital ya Taifa ya Muhimbili Mloganzila, haki ya nani mmebadilisha maisha yangu tayari ndani ya wiki moja tu. Mkurugenzi Mkuu wa Muhimbili Profesa Janabi kongole sana,” ameandika Msechu.