Mufti Zubeir awataka Waislamu kujikinga na corona

Mufti Zubeir awataka Waislamu kujikinga na corona

Muktasari:

  • Mufti wa Tanzania Sheikh Abubakar Zubeir amewataka Waislamu kuzingatia maagizo yanayotolewa na wataalam wa afya kuhusu kujikinga na maambukizi ya magonjwa mbalimbali ukiwemo Covid-19 unaosababishwa na virusi vya corona.

Dar es Salaam. Mufti wa Tanzania Sheikh Abubakar Zubeir amewataka Waislamu kuzingatia maagizo yanayotolewa na wataalam wa afya kuhusu kujikinga na maambukizi ya magonjwa mbalimbali ukiwemo Covid-19 unaosababishwa na virusi vya corona.

Ameeleza hayo leo jioni Ijumaa Mei 14, 2021 katika baraza la Idd lililofanyika katika viwanja vya Karimjee mkoani Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali akiwemo Rais Samia Suluhu Hassan.

“Kuna jambo limezungumzwa katika salamu zetu za baraza kuhusu afya. Afya ndio itakayotufanya tuweze kuswali, kufanya ibada, kushughulika masuala ya kiuchumi, kufanya biashara. Uislamu unasema kuilinda afya ni jambo la lazima, tufuate maelekezo ya wataalam wa afya kwa ajili ya kujikinga na magonjwa mbalimbali ikiwemo corona.”

“Tusipuuze hata kidogo, tukae mbalimbali, kuvae barakoa, kunawa mikono kwa maji tiririka. Mtu anayejiachia ili aangamie anakuwa amejiangamiza mwenyewe, ugonjwa ukitokea tuangalie masharti na tunajitibu namna gani,” amesema.