Mume adaiwa kumuua mkewe wivu wa mapenzi ukitajwa

Mume adaiwa kumuua mkewe wivu wa mapenzi ukitajwa

Muktasari:

  • Mkazi  wa kata ya Malezi wilayani Handeni mkoani Tanga,  Nassoro Mustapha anatuhumiwa kumuua mkewe kwa kumkata na panga sehemu mbalimbali mwilini ikielezwa  sababu  ni wivu wa mapenzi.

Handeni. Mkazi  wa kata ya Malezi wilayani Handeni mkoani Tanga,  Nassoro Mustapha anatuhumiwa kumuua mkewe kwa kumkata na panga sehemu mbalimbali mwilini ikielezwa  sababu  ni wivu wa mapenzi.

Tukio hilo limetokea jana Agosti 3, 2021 katika mtaa wa Kwamaraho iidaiwa  kuwa mwanaume huyo alikuwa na ugomvi  na mkewe na ndio uliomrudisha nyumbani.

Dada wa marehemu,  Rehema Hemed amesema wanahisi tukio hilo limetokana  na wivu wa mapenzi kwa sababu  wanandoa hao walikuwa na ugomvi na kwamba  shemeji yake alikuja nyumba wakiwa hawapo na kumshambulia mdogo wake.

 "Nilikuwa kazini nikapata taarifa kwamba mdogo wangu amekatwa panga na mumewe, tulifika nyumbani na kumkuta amejeruhiwa mwili lakini alifariki tukiwa  njiani kumpeleka  hospitali, "amesema Rehema.

Rehema amesema ndugu yake amefariki akiwa ni ujauzito wa  miezi sita au  na ameacha  mtoto wa miaka mitatu.

Diwani wa Malezi,  Shabani Kitombo amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa ni  la pili katika mtaa huo mwaka huu.

"Nilivyoelezwa huyu binti amechalazwa mapanga maeneo ya shingoni na mumewe na chanzo cha ugomvi ndugu zake wanahisi ni sababu za mapenzi na mhusika anaendelea kutafutwa baada kukimbia, " amesema Kitombo.

Juhudi za Mwananchi Digital  kumtafuta Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga,  Blasius Chatanda kuzungumzia  tukio hilo zinaendelea.