Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Mwalimu, mwanafunzi wakutwa wameuawa ndani ya nyumba

Mwalimu wa Shule ya Msingi Mbugani Herieth Lupembe enzi za uhai wake

Muktasari:

  • Katika tukio hilo, mtoto mdogo wa miaka mitano wa mwalimu huyo amejeruhiwa na sasa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya.

Mbeya. Mwalimu wa Shule ya Msingi Mbugani Kata ya Kiwanja, Herieth Lupembe na binti aliyekuwa akiishi naye ambaye ni mwananfunzi wa Kidato cha kwanza, Tatizo Haonga (16) wamekutwa wameuawa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali kichwani na mwilini.

Mauaji hayo yamefanyika ndani ya nyumba aliyokuwa wakiishi pamoja na mtoto wa mwalimu huyo mwenye umri wa miaka mitano.

Mwanafunzi aliyeuawa pamoja na mwalimu huyo alikuwa anasoma katika  Shule ya Sekondari Isenyela wilayani Chunya.

Katika tukio hilo, Haris Daud (5) anayesoma darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Kengold amejeruhiwa na sasa anapatiwa matibabu katika Hosptali ya Rufaa Kanda ya Mbeya.

Inaelezwa kuwa tukio hilo limetokea jana Jumapili Machi 31, 2024 na majirani ndiyo waliobaini baada ya kutomuona mwalimu huyo akienda kanisani huku duka lake likiwa limefungwa, jambo ambalo si la kawaida.

 Akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu Aprili mosi, 2024 jirani wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Merry Joel amesema walipoona duka limefungwa, waliamua kupiga simu ya mwalimu huyo ikawa inaita bila majibu.

“Tukaamua kufuatilia nyumbani kwake ndipo tukabaini kuwa ameuawa ndani kwake pamoja na huyu mtoto aliyekuwa anakaa naye. Mtoto wake tumekuta ameumizwa,” alidai jirani huyo na kuongeza; 

“Tulipofika nyumbani kwake tulishtuka kukuta bidhaa za dukani zikiwa nje, umbali wa mita 50 kutoka nyumbani kwake na bidhaa hizo alikuwa ameziagiza kutoka mjini Mbeya.”

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga alipotafutwa kuzungumzia tukio hilo, simu yake ya kiganjani iliita bila majibu.

Akizungumzia tukio hilo, Mwenyekiti  wa Kijiji cha Mbugani, Gideon Kinyamagohaamesema baada ya kupokea taarifa za tukio amewasiliana na Jeshi la Polisi na askari wamefika na kufanya uchunguzi wa awali kisha kuchukua miili kwenda kuihifadhi katika Hospitali ya Wilaya ya Chunya kwa uchunguzi zaidi na mtoto majeruhi amepelekwa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya.

Mzazi wa mwanafunzi aliyeuawa, Faxson Simchimba amesema mwanawe alianza kuishi na mwalimu huyo baada ya kufaulu darasa la saba.

“Mwalimu alimchukua mwanangu ili aishi kwake kwa sababu ni jirani na shuleni alikokuwa anasoma, nini kimetokea hadi wameuliwa hata sijui,” amesimulia mzazi huyo.

Mwenyekiti wa Mtaa wa wa Mbugani, Chambo Mpigauzi amesema hajawahi kusikia kama mwalimu huyo alikuwa na tofauti na mtu, bali alikuwa na uhusiano mzuri na jamii na ameshangazwa na mauaji hayo.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Chunya, Bosco Mwangindea ambaye ni Diwani wa Mbugani, amesema hilo ni tukio la kwanza kutokea kwenye kata yake.

“Hatujawahi kushuhudia mauaji ya kikatili namna hii, tunalaani vikali wote waliotekeleza mauaji haya na tunaliomba Jeshi la Polisi lifanye haraka uchunguzi,” amesema diwani huyo.