Nape ataka mashirika ya Posta Tanzania na Kenya kufanya biashara kidigitali

Postamasta Mkuu wa Shirika la Posta Tanzania, Macris Mbodo

Muktasari:

Waziri wa  Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye ameyataka mashirika ya  Posta Tanzania na Kenya kuhakikisha wanafanya biashara ya usafirishaji kwa njia ya kidigitali zenye kukidhi vigezo vya kimataifa lengo likiwa kuwavutia wananchi wa nchi hizo  kufanya biashara na mashirika hayo.

Arusha. Waziri wa  Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye ameyataka mashirika ya  Posta Tanzania na Kenya kuhakikisha wanafanya biashara ya usafirishaji kwa njia ya kidigitali zenye kukidhi vigezo vya kimataifa lengo likiwa kuwavutia wananchi wa nchi hizo  kufanya biashara na mashirika hayo.
Hayo yamesemwa leo Novemba 1 jijini Arusha na Naibu Waziri wa  Habari, Mawasiliano  na Teknolojia  ya Habari, Kundo Mathew kwa niaba ya Waziri Nape  katika hafla ya uzinduzi  wa  biashara  ya kuvuka mpaka kwa njia ya kidigitali kati  ya Tanzania  na Kenya  iliyofanyika katika mpaka wa  Namanga.
Amesema kuwa,uwepo wa biashara hiyo kwa nchi hizo  utabadilisha muundo  mzima wa Kidigital katika  kufanya usafirishaji  wa vifurushi  hivyo kwa wateja  wake  na kuwafikia  ndani ya muda  sambamba na kuokoa gharama zilizokuwepo  hapo awali.
Nape amesema kuwa, uwepo wa  mfumo huo utaongeza  fursa za ajira kwa vijana walio wengi   kwani kwa kufanya hivyo wanaendana na  mabadiliko ya sayansi  na teknolojia.
"Niwaombe sana muendelee kuwa wabunifu zaidi  ili kuondoa usumbufu  uliokuwepo awali  kutokana na mzunguko mrefu uliokuwepo wa  kufikiwa  na huduma hizo.  Nawaomba sana mashirika yote mawili muendelee kupata uzoefu zaidi  kutoka nchi zingine sambamba na kuiga  yale mazuri yaliyopo katika nchi zingine,"amesema.
Postamasta Mkuu  wa Shirika la Posta Tanzania, Macris  Mbodo amesema kuwa, lengo la uzinduzi wa biashara ya kuvuka mpakani  (Cross Border Business) kati ya Tanzania na Kenya ni kurahisisha utoaji wa huduma za usafirishaji  wa  vifurushi, vibeto na mizigo  kwa wananchi wake na kuweza kuondokana na changamoto  mbalimbali.
Mbodo amesema kuwa, zamani ilikuwa inawalazimu mizigo kwenda hadi jijini Da es Salaam ambapo ilikuwa inachukua  muda  mrefu na gharama pia, ila  kwa sasa hivi  itawasaidia kurahisisha gharama na kuweza kuchukua  mizigo hiyo hapa hapa karibu ndani ya muda  mfupi.
"Rais Samia Suluhu Hassan amefungua nchi yetu kwa kuweza kufanya biashara mbalimbali hivyo tumeona tuunge mkono jitihada za serikali kwa kuimarisha  usafirishaji  wa  vifurushi mipakani  na kuweza  kuokoa gharama zilizokuwepo hapo awali na tumejipanga kuhakikisha huduma zetu zinawafikia wananchi waliopo na sio wananchi wazifuate huduma,"amesema.
Kwa upande wake  Postamasta Mkuu wa  Shirika la Posta  Kenya,Dan  Kagwe amesema kuwa,miaka iliyopita tulikuwa hatuna mipaka bali tulikuwa majirani na tulikuwa tunaishi kwa amani na upendo mkubwa hivyo uwepo mipaka  umesaidia sana kuongeza  ushirikiano  zaidi  kwa wananchi wa nchi Kenya na Tanzania.
"Uwepo wa uzinduzi huu wa biashara ya kuvuka  mpakani  utasaidia  sana kufanya biashara zetu ziwe  za mashirikiano  zaidi na kuweza kukuza  uchumi  wa  nchi zetu."amesema Kagwe.
Katibu Mkuu wa Umoja wa  Posta Afrika (PAPU), Sifundo Chief Moyo  amesema kuwa,  uwepo wa ushirikiano huo kati ya nchi zote mbili  itasaidia kuokoa muda na gharama walizokuwa  wanatumia wananchi katika kupata huduma hizo kwani kwa sasa hivi watachukulia  napa hapa  mpakani tofauti na hapo  awali.