Necta yaleta mfumo mpya utunzaji taarifa za wanafunzi
Muktasari:
Msonde amesema mfumo huo utawasajili wanafunzi wa shule za msingi na kupewa namba maalumu watakazotumia ngazi zote za elimu.
Dar es Salaam. Baraza la la Mitihani la Tanzania (Necta), limezindua Mfumo wa Kutunza Taarifa za Wanafunzi wa Shule za Msingi (PRem), utakaowezesha baraza hilo kupata takwimu mbalimbali za usajili wa upimaji darasa la nne na kumaliza elimu ya msingi.
Mfumo huo umezinduliwa leo, Mei 5, 2018 na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk Leonard Akwilapo na ulifanyika katika kituo cha kusahihisha mitihani, Mbezi.
Katika uzinduzi huo Katibu Mtendaji wa Nacte, Dk Charles Msonde amesema kupitia mfumo huo wanafunzi wa shule za msingi watasajiliwa na kupewa namba maalumu za utambulisho watakazotumia kwenye ngazi zote za elimu.
Amesema mfumo huo pia, utamwezesha mwanafunzi kuhama shule moja kwenda nyingine ndani ya kata, halmashauri au mkoa na atakuwa akiidhinishwa kwa wakati na maofisa elimu kupitia PRem.
Kwa upande wake, Dk Akwilapo ameshukuru ubalozi wa Sweden nchini kwa kufadhili mradi huo utakaosaidia kufuatilia taarifa za matokeo ya mwanafunzi katika ngazi ya shule, halmashauri, manispaa ya jiji, mkoa na kitaifa.
"Mfumo huu una umuhimu mkubwa kwa ajili ya maendeleo ya sekta ya elimu nchini.Sasa hivi wanafunzi wote wa shule za msingi watapatikana katika kanzidata moja,"amesema Dk Akwilapo.