Okay! Kwa Wasafi sawa Gigy Money hajajifunza?

Muktasari:
- Any way, nimesikia TCRA wamekaa, wakafikiria na kulitazama kwa jicho la tatu tatizo la Wasafi. Wamejiridhisha kuwa walikurupuka na kuamua kutengua maamuzi yao katili ya mwanzo. Habari njema.
Niaje waungwana. Naona mjini sasa zimeanza kuonekana sura zenye nuru. Au bado mnasafisha makovu ya Njaanuari? Hakuna namna shida tumeumbiwa sisi sio ngedere wala tumbili. Umenisoma?
Ndio hivyo. Tumeamua kuishi namna tunavyoishi. Ni wewe mwenyewe ukitaka kuishi tofauti itakuwa. Hakuna mwingine wa kukufanya wewe uwe tofauti au uwe vile utakavyo unachotakiwa kujua ni kwamba, hatuishi mara mbili.
Mwezi umeingia na shoo ya kizazi kipya cha kale pale mitaa ya Dodoma Town. Nikisema cha kale nieleweke kwamba, siwaongelei kina Zuchu, namuongelea mama yake mdogo kama ni Jide na wenzake.
Kizazi kipya cha kale, ukiwatazama hata mitandaoni kinachowatofautisha na kina Lavalava ni makunyazi usoni, itambi na aina ya mavazi pamoja na pozi katika maongezi. Kina Lavalava wana swaga new model.
Uvaaji wa Lavalava hutouona kwa Mchizi Mox, wa Rayvanny haupo ndani ya Mkoloni wa Wagosi wa Kaya. Kuna uzi mwembamba unaotenganisha kizazi kile kipya cha kale na hiki kipya cha sasa kina nongwa.
Na kinachotenganisha ni mavazi, ugumu wa ngozi na ukubwa wa matumbo kifupi ni ule mwonekano tu. Na hiki kilikuwepo pia enzi za kina Ally Choki na kina Tx Moshi William, nao walikuwa kama hivi sasa TID na Marioo.
Wazee wetu nao walitofautiana pigo za mionekano zaidi ya hapo wote akili zilikuwa moja. Kwenye sanaa ya muziki ndio sehemu pekee yenye akili moja ila mavazi tofauti. Yes namaanisha.
Tofauti inakuja kwenye mahitaji na hali ya mazingira, zamani Ferouz angepanga foleni kwa Mdosi Kariakoo leo Diamond, anaangalia miamara kwa mtandao tu.
Mengineyo ni yale yale, umiliki wa pisi kali toka enzi za kina Mbaraka, Marijani na Chidumule Cosmas ndio maana ya muziki. Maisha ya muziki na madem ni pete na kidole. Yes ndio ukweli.
Usilete stori kwamba madogo wa sasa wamewekeza akili kwa pisi kali hapana! Long time kitambo wanamuziki na sanaa wamejenga ‘bondi’ na pisi, kifupi hata pisi zinajua hilo kwamba wapo kwa ajili yao.
Wateja wakubwa wa muziki ni madem, elewa mjomba masela wengi masnichi tu hamna kitu. Dem anaweza kumlilia msanii jukwaani kwa kusuuzwa moyo, masela watakurusha makopo jukwaani kisa totozi.
Ili tuelewane mtafute mkazi wa Dom, ambaye atakuwepo eneo la tukio au maeneo ya bata siku ya shoo. Mbugi like likiisha wote wataelekea Pestana, Royal Village sijui na maeneo yote ya bata batani.
Mzoefu wa bata utaona tu namna malipo yao ya shoo yakiishia kwenye mitungi na pisi kali. Msanii asiyetumia pesa kwa pisi ujue marioo. Lakini katika uhalisia wao utaona unyambisi wao wa matumizi. Kama vichaa.
Hakuna hata mmoja kati ya wale wote waliopo huko wa kukumbuka suala la hatimiliki. Sijui urasimishaji wa kazi za sanaa yao na udhibiti wa malipo yao kila mtu anajijali yeye, miwani nyeusi, simu pana ya kuchat na vicheche.
Watatoka uwanjani kwenye shoo yao hiyo wote wataenda baa zikigongwa ngoma zao huko wataishia kukenua meno, akili zote kwenye pisi. Bila kujali hizo baa zinavutia watu kwa huduma pamoja na muziki wao.
Wamiliki wa hizi baa enzi zao walikuwa mashabiki wa muziki wao na pengine walikuwa vyuoni au sekondari. Leo hii wamemaliza masomo wamefungua baa zao, wasanii wanabaki kuwa wateja wao vilevile tu.
Hata wasanii wa sasa ni wachache wenye uwekezaji wa kueleweka wengi huwaza kupush mikoko, kuwekeza katika nywele kichwani na tattoo mwilini, kutinga pamba kali na kukamatia madem flan hivi..
Wanachokosa ni usimamizi mzuri na hata wenye usimamizi, hao wasimamizi wanawaza matumbo yao kwanza. Kina Aslay na wenzake wanaweza kuwa ni mifano hai. Ujanja na uhuni umekuwa mwingine sana.
Sometime kuwaongelea hawa masela ni jambo gumu kinoma. Huko Dom wapo na Serikali yote, lakini watarudi hapa Daslama mjini wakiwa walewale juu ya matatizo yao. Nani wa kuwasemea? Hakuna.
Any way, nimesikia TCRA wamekaa, wakafikiria na kulitazama kwa jicho la tatu tatizo la Wasafi. Wamejiridhisha kuwa walikurupuka na kuamua kutengua maamuzi yao katili ya mwanzo. Habari njema.
Wakati TCRA wakipunguza adhabu kwa Wasafi Tv, naona Basata kama wao ni watu wa kufuata maamuzi ya wenzao. Hawajiamini au hawajui wanalofanya miaka yote mpaka watu wapige kelele.
Hata Waziri wa Habari Innocent Bashungwa, toka mwanzo maelezo yake yamejikita kwenye Wasafi Tv tu bila kuongelea suala la Gigy Money kama msanii. Dada kama vile alitengwa mpaka watu wapige kelele?
TCRA walikuwa sahihi walichofanya, Basata walikurupuka walikuwa na muda wa kujiuliza. Kosa la Wasafi kwa TCRA halihusiani na Gigy Money hata kama kweli alivaa mavazi yasiyofaa.
Kama Gigy alikuwa amevaa vibaya time ile usiku jukwaani, tena ukumbini tatizo liko wapi? Ila runinga kuonyesha ‘laivu’ lingekuwa kosa. Kama kweli wale Basata wanaamini lile ni kosa basi hawajui dunia ya leo.
Kwenye vishughuli vya mitaani humu, tena mchana kweupee ujinga ni mwingi zaidi. Hatuna maana ya kuhalalisha makosa ila hatuungi mkono papara za Basata. Mlikurupuka kumfungia Gigy.
Makosa ya Basata yamewafikisha hapa , huwezi kuona wasanii wakiongea na Bashungwa wala Dk Abbas kuhusu haki zao wataishia kupiga nao picha na stori za uongo na ukweli basi imeisha hiyo. Lakini huku mitaani huponda na kulalamika balaa.
Wasanii wa kale na sasa wapo wachache mno ambao wana uthubutu wa kuongelea mahitaji na haki zao za msingi kwa vyombo husika. Wengi wao ni kama wanasubiri ifike kiama wasepe.