Pele afikisha miaka 80 akiwa amejitenga

Mfalme wa soka duniani, Pele wa Brazil

Muktasari:

Pele aliiongoza Brazil kutwaa Kombe la Dunia mwaka  1958, 1962

na 1970 na hivyo kuweka rekodi ya kuwa mwanasoka pekee duniani aliyeweza kutwaa ubingwa huo mara tatu..

Sao Paulo, Brazil. Mfalme wa soka duniani, Pele wa Brazil jana Ijumaa amefikisha umri wa miaka 80, lakini bila ya shamrashamra.

Mshambuliaji huyo aliyetwaa Kombe la Dunia mara tatu,

amejitenga akiwa na watu wachache wa familia yake nje ya jiji la Sao Paulo, ambako anatazamiwa kumiminiwa salamu za pongezi kutoka kwa wachezaji, mashabiki, watu maarufu na wanasiasa.

Msemaji wake wa muda mrefu, Pepito Fornos, alisema Pele alitarajiwa kusherehekea sikukuu yake ya kuzaliwa katika jumba lake lililoko ufukweni katika jimbo la Sao Paulo, ambako amekuwa akiishi tangu kuibuka kwa ugonjwa wa virusi vya corona, Covid-19. Gwiji huyo wa soka pia ana makazi Santos na Sao Paulo.

“Atakuwa na familia yake tu. Hakuna sherehe kabisa,"alisema Fornos alipoongea na shirika la habari la AP.

“Imekuwa hivyo wakati wote maishani mwake.”

Fornos alisema Pele hazungumzi hadharani kwa sababu

bado anaomboleza kifo cha kaka yake Jair, ambaye alifariki mwezi Machi kwa ugonjwa wa saratani.

Pele anaongoza kwa ufumaniaji nyafu ndani ya timu ya

taifa ya Brazil baada ya kutundika mabao 77,ingawa Neymar anakaribia rekodi hiyo akiwa amefunga mabao 64.

Lakini mshambuliaji huyo wa klabu ya Paris Saint- Germain ameachwa mbali linapokuja suala la kutwaa Kombe la Dunia, ambalo Pelé alitwaa mwaka 1958, 1962 na 1970.

Hakuna mchezaji mwingine duniani aliyefikia rekodi

hiyo.