Profesa Mbarawa aanza na Tanroads

Muktasari:

  • Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Profesa Makame Mbarawa ameanza kazi kwa kuwataka Wakala wa Barabara Nchini (Tanroads) kutafuta kifaa cha kupimia ubora wa barabara nchini na viwanja vya ndege.

Dodoma. Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Profesa Makame Mbarawa amewaagiza Wakala Barabara Nchini (Tanroads) kununua vifaa vya kupima ubora wa viwanja vya ndege na barabara nchini badala ya kupima kwa kuangalia kwa macho.

Profesa Mbarawa ameyasema hayo leo Jumatatu Septemba 13, 2021 wakati wa hafla ya utiliaji saini wa mkataba wa ujenzi wa Uwanja wa Kimataifa wa Msalato jijini hapa, muda mfupi baada ya kuapishwa na Rais Samua Suluhu Hassan mkoani humo.

Mkataba huo ulisainiwa na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Nchini (Tanrods) Rogatus Mativila na Kampuni iliyoshinda zabuni ya kujenga uwanja huo ya Synohydro Company Limited.

Awamu ya kwanza ya ujenzi wa Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Msalato jijini Dodoma utakaowezesha abiria milioni 1.5 kuhudumiwa kwa mwaka utakamilika baada miezi 36.

Akizungumza Profesa Mbarawa amesema wabunge wamekuwa wakilalamikia kuhusu barabara zinazoharibika baada ya muda mfupi.

“Lakini tukinunua vifaa tutakuwa tunajihakikishia kazi tunayofanya inaenda kwa viwango vya juu.  Najua Tanroads mnauwezo mkubwa lakini mkitafuta vifaa vya teknolojia ya juu naamini mtafanya kazi,”amesema

Amesema atalisimamia hilo kwa kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja na nusu kifaa hicho kinafika nchini na hivyo kila barabara inayokamilika iweze kupitishiwa Road Scanner.

Aidha, ameutaka wakala huo kubadilika kwa kufanya kazi kwa kasi kubwa, barabara ziwe za viwango vikubwa na zinazodumu kwa muda mrefu.

Pia amewataka kuangalia upya gharama za ujenzi wa barabara ili zipungue bila kuathiri ubora wake kutoka gharama za sasa za Sh1.5 kwa kilometa moja.