Rais Samia aanza ziara ya siku nne Mbeya

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan

Muktasari:

Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameanza ziara ya siku nne jijini Mbeya yenye lengo la kukagua na kufungua miradi mbalimbali ya maendeleo jijini humo.

Mbeya. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Ijumaa Agosti 5, 2022 ameanza ziara ya kikazi ya siku nne katika Mkoa wa Mbeya.

Katika ziara hiyo, Rais Samia atakagua na kufungua miradi mbalimbali ya maendeleo katika wilaya za Mbeya, Chunya, Mbarali, Kyela na Rungwe.

Rais Samia atakagua na kuzindua Mradi wa Maji wa Shongo -Igale unaosimamiwa na Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Mkoa wa Mbeya (Mbeya-Uwwas).

Pia atafungua, jengo la Mama na Mtoto Hosptali ya Rufaa ya Wazazi Meta, Mradi wa Jengo la ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya na kuweka mawe ya msingi.

Rais mara baada ya kuzindua mradi  wa Maji  Shongo -Igale atasalimia wananchi wa mamlaka mji mdogo wa Mbalizi na baadaye wajenzi katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa na kuzungumza na watumishi.

Awali, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema kuwa mbali na Rais kuzindua mradi wa Maji wa Shongo -Igale pia ametoa zaidi ya Sh 250 bilioni kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi  mkubwa wa maji wa mto Kiwira utakaoondoa hadha ya maji katika Mkoa wa Mbeya.

Aidha, Rais Samia anatarajia kufunga maonyesho ya sikukuu ya wakulima nanenae Agosti 8, 2022 jijini humo.